Wanafunzi 37 wauawa shambulio la waasi nchini Uganda

Muktasari:

  • Takribani wanafunzi 37, wameuawa katika shambulio lililofanywa na waasi katika shule moja nchini Uganda, ambayo ipo karibu na mpaka wa DRC.

Wanafunzi takribani 37 wameuawa katika shambulio la waasi katika shule moja nchini Uganda karibu na mpaka wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Kwa mujibu taarifa za kipolisi nchini humo kundi la wapiganaji lenye uhusiano na ISIL (ISIS) limewauwa wanafunzi takribani 37 katika shambulio dhidi ya Shule ya Sekondari ya Lhubirira magharibi mwa Uganda.

Kundi la Uganda Allied Democratic Forces (ADF) lenye makao yake makuu mashariki mwa DRC ambalo linashirikiana na ISIL, limeshambulia shule hiyo huko mjini Mpondwe, na kuchoma bweni pamoja na kupora chakula jioni ya Ijumaa.

“Hadi sasa maiti zaidi ya 37 zimeopolewa shuleni hapo na watu zaidi ya nane wamejeruhiwa kutokana na shambulio hilo,” wamesema Police wa Uganda kupitia mtandao wa Twitter.

“Mamlaka haikubainisha ni wanafunzi wangapi walikuwa miongoni mwa waathiriwa wa shambulio hilo”

Hata hivyo, gazeti la Daily Monitor, limenukuu baadhi ya vyanzo vya usalama nchini humo ambavyo havikutajwa majina, vikisema washambuliaji wa Allied Democratic Forces (ADF) wamewateka nyara watu wengine kadhaa kabla ya kukimbia.

Msemaji wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi Uganda, Felix Kulayigye amesema vikosi vyake vinafanya jitihada za kuwafuatilia washambuliaji kwa lengo la kuwaokoa wale waliotekwa nyara na washambuliaji hao waliokimbia kuelekea Hifadhi ya Taifa ya Virunga nchini DRC.

Mnamo 2021, Uganda ilianzisha mashambulizi ya anga na mizinga nchini DR Congo dhidi ya ADF, na kundi hilo pia linaaminika kuhusika na mauaji ya watu 36 mwezi Machi wakati wa shambulio la usiku katika kijiji cha Mukondi, mashariki mwa DRC.

Endelea kufuatili mitandao ya Mwananchi Digital