Afariki baada ya kukanyagwa na tembo
Muktasari:
Dayness Josephat (58) mkazi wa kata ya Maore Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro amefariki baada ya kukanyagwa na tembo wakati akienda shambani kwake.
Same. Dayness Josephat (58) mkazi wa kata ya Maore Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro amefariki baada ya kukanyagwa na tembo wakati akienda shambani kwake.
Mwenyekiti wa kitongoji cha Igoma, Julius Mtegwa amethibitisha kutokea kwa tukio leo Jumatano Mei 26, 2021 saa 2 asubuhi.
"Hili tukio limetokea asubuhi leo wakati huyu mama na wenzake wakienda shambani, walikuwa watatu lakini wawili walifanikiwa kukimbia. Tembo amemrarua kila mahali hadi utumbo wake wote umetoka nje," amesema Mtegwa
Mei 23, 2021 naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Marry Masanja alipofanya ziara wilayani Same na Mwanga alisema wizara hiyo imeweka mkakati wa namna ya kudhibiti tembo kutoingia kwenye makazi ya watu ikiwa ni pamoja na kuweka mizinga ya nyuki kwenye maeneo yote yalizozunguka hifadhi pamoja na kupanda miti.