Ahukumiwa kifungo miaka 40 kwa kuwadhalilisha watoto kingono
Muktasari:
Mkazi wa Isevya, Manispaa ya Tabora, Francis Julius Matiko (19) amehukumiwa kutumikia kifungo cha miaka 40 jela baada ya kutiwa hatiani kwa makosa mawili tofauti ya ukatili wa kingono kwa watoto.
Tabora. Mkazi wa Isevya, Manispaa ya Tabora, Francis Julius Matiko (19) amehukumiwa kutumikia kifungo cha miaka 40 jela baada ya kutiwa hatiani kwa makosa mawili tofauti ya ukatili wa kingono kwa watoto.
Hukumu hiyo, imetolewa leo Ijumaa Oktoba 28, 2022 na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Tabora, John Mdoe baada ya kuridhika na ushahidi uliotolewa na mashahidi watano wa upande wa mashtaka wakiwemo waathirika wa ukatili huo.
Upande wa mashitaka katika shauri hilo ukiongozwa na wakili Joseph Makeno, uliiambia mahakama hiyo kuwa mshtakiwa alitenda makosa hayo mawili, Mei 22, 2021 kinyume na kifungu namba 138 C (1) (a) na Kifungu kidogo (2) (b) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu.
Amesema kuwa siku hiyo katika Kata ya Isevya, Manispaa ya Tabora na kwa nyakati tofauti, mshtakiwa aliwashika maungoni ikiwemo sehemu zao za siri watoto wawili wa kike ambao majina yao yanahifadhiwa.
Wakili Makeno ameiambia mahakama hiyo kuwa ili kufanikisha shambulizi hilo la kingono kwa watoto hao mshtakiwa alikuwa akiwalaghai kwa kuwapatia fedha kati ya Sh500 hadi Sh1,000 au kinywaji aina ya juisi.
Ameongeza kuwa awali alimchukua mtoto wa kwanza mwenye umri wa miaka sita na kumpeleka chumbani mwake na kumlaza kitandani na kuanza kumshika makalio, manyonyo na sehemu za siri, ukeni.
Upande wa Jamhuri umeongeza kuwa ikiwa haitoshi na bila woga mshtakiwa alimchukua mtoto wa pili na kumpeleka chooni na kuanza kumfanyia vitendo hivyo vya ukatili wa kingono.
Akitoa utetezi wake, Francis Matiko amedai kuwa amefunguliwa kesi hiyo kwa hila kutokana na ugomvi kati yake na shahidi wa kwanza ambaye ni bibi wa mmoja wa wahanga kwamba alikuwa akimtaka kimapenzi bila mafanikio.
Matiko ameongeza katika utetezi wake kuwa bibi huyo alikuwa akimfuata amevaa khanga moja lakini alimkatalia ndipo akamwambia kwamba atamkomesha.
Katika hukumu hiyo hakimu Mdoe, amesema utetezi wa mshtakiwa hauna nguvu kutokana na ukweli kwamba aliyemtaja kwamba alimtaka kimapenzi ni miongoni mwa mashahidi lakini hakuweza kumuuliza swali wakati wa shauri.
Ameongeza kuwa mshitakiwa amewasilisha utetezi wake muda ambao sio mwafaka kwani ameutoa baada ya kujitafakari.
Akitoa uamuzi wa kesi hiyo hakimu Mdoe, amesema kwa kuzingatia ushahidi wa waathirika wa kumtambua mshtakiwa pasipo shaka yoyote, mahakama inamhukumu kutumikia kifungo cha miaka 20 jela kila kosa ambacho ndicho kima cha chini cha adhabu .
Mahakama pia imemtaka mshitakiwa kuwalipa watoto hao wawili fidia ya Sh100,000 kila muathirika, Hata hivyo atatumikia kifungo cha miaka 20 jela kwa vile adhabu hizo, zinaenda pamoja.