Ajali yaua watu watano Tabora

Muktasari:

Watu watano wamefariki dunia na wengine watatu wamejeruhiwa baada ya magari mawili kugongana uso kwa uso katika Kijiji cha Tura wilayani Uyui mkoani Tabora.

Tabora.   Watu watano wamefariki dunia na wengine watatu wamejeruhiwa baada ya magari mawili kugongana uso kwa uso katika Kijiji cha Tura wilayani Uyui mkoani Tabora.

Taarifa iliyotolewa leo Jumatatu Februari 14, 2022 na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora (RPC), Richard Abwao imesema kuwa ajali hiyo imetokea jana usiku katika kizuizi cha mazao ya misitu.

Kamanda Abwao amesema kuwa gari ndogo aina ya aina ya Toyota Rav4 ambayo iliyokuwa inatoka Tabora kuelekea Dar es Salaam iligongana uso kwa uso na lori.

Kamanda Abwao amesema katika ajali hiyo watu wanne walifariki papohapo huku mmoja akifariki baada ya kufikishwa katika Hospitali ya Mkoa wa Tabora.

Amesema kuwa miili ya marehemu hao imehifadhiwa katika Hospitali ya Mkoa wa Tabora.

Kamanda Abwao amesema chanzo cha ajali hiyo ni uoni hafifu wa kizuizi cha mazao ya misitu kilichowekwa katika barabara.