Bakwata Kilimanjaro kuchinja ng’ombe 500 Eid Al-Adha, kugawa kwa wahitaji
Katibu wa Baraza kuu la Waislam(Bakwata) mkoa wa Kilimanjaro Awadhi Lema, akizungumzia maandalizi ya Sikukuu ya Eid. Picha na Janeth Joseph
Muktasari:
- Katibu wa Bakwata mkoani humo, Awadhi Lema amesema mbali na shughuli ya kuchinja pia, kutakuwa na mahubiri mbalimbali ya amani katika misikiti yote ya mkoa huo kwa ajili ya kuliombea Taifa.
Moshi. Ikiwa zimesalia siku tano kuelekea sikukuu ya Eid Al-Adha, Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata) Mkoa wa Kilimanjaro limepanga kuchinja ng'ombe zaidi ya 500 kusherekea pamoja na wenye uhitaji mkoani humo.
Akizungumzia maandalizi ya sherehe hizo leo Mei 22, 2026, Katibu wa Bakwata mkoani humo, Awadhi Lema amesema mbali na shughuli ya kuchinja, pia, kutakuwa na mahubiri mbalimbali ya amani katika misikiti yote ya mkoa huo kwa ajili ya kuliombea Taifa.
Aidha, amewataka waumini wa dini hiyo kushiriki kwa amani na utulivu katika maadhimisho ya sikukuu hiyo muhimu kwa Waislamu huku akihimiza mshikamano na upendo miongoni mwa wanajamii.
“Maandalizi yanaendelea vizuri na viongozi wa dini watatumia siku hiyo kuhubiri umuhimu wa kudumisha amani, upendo, umoja na maadili mema katika jamii pamoja na kuliombea Taifa letu,” amesema.
“Zipo nchi ambazo amani iliwahi kupotea mpaka leo wanateseka kuitafuta, hivyo suala la amani litahubiriwa katika misikiti yote kutokana na viashiria ambavyo tumeviona.”
Pamoja na mambo mengine, amesema siku hiyo watajumuika na kusherekea pamoja na watoto yatima na wale wanaotoka katika mazingira magumu kama sehemu ya kuwapa faraja.
“Eid hii ni ya kuchinja na kutoa sadaka, hivyo tunazo ng'ombe 500 na tutazichinja baada ya sala kwa ajili ya kugawa nyama kwa wasiojiweza, yatima na wale ambao hawana uwezo lakini na hata kwa wale wanaojiweza, sadaka huwa haichagui,” amesema Lema.
Kwa upande wake, Kadhi wa mkoa huo, Hussein Chifupa ameitaka jamii kuungana na wasiojiweza kuonyesha upendo siku hiyo ili waweze kupata thawabu kwa Mungu.
Amesema: “Katika sikukuu hii tunajifunza utii kwa Mwenyezi Mungu kwamba mwanadamu anatakiwa amtii Mola wake na kumuabudu.”