Bandari Bagamoyo yawagawa vigogo CCM

Muktasari:

  • Ujenzi wa bandari ya Bagamoyo umewaibua makada wa CCM ambao kila mmoja amekuja na mtazamo wake.

Dodoma. Ujenzi wa bandari ya Bagamoyo umewaibua makada wa CCM ambao kila mmoja amekuja na mtazamo wake.

Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara Philip Mangula na mbunge wa Mtama, Nape Nnauye wamekuwa na mtazamo tofauti lakini wote wakijificha katika Ilani ya uchaguzi ya 2020-2025.

Mzee Mangula alikaririwa na moja ya vyombo vya habari vya chama hicho akitaka Watanzania wasisumbuke na habari za Ujenzi wa bandari hiyo.

"Watanzania waache kuhangaika na upotoshaji wa ujenzi wa bandari ya Bagamoyo kwa kuwa haimo katika Ilani, kilichomo ni Ujenzi wa gati," alisema Mangula.

Mkongwe huyo amewataka Watanzania wamuache Rais Samia Suluhu Hassan kuendelea na kazi yake ya kuwatumikia wananchi.

Hata hivyo Nape ameandika katika mtandao wake akihoji kuhusu miradi mikubwa ambayo imewahi kujengwa wakati haikuwa kwenye Ilani.

"Najiuliza tu kimyakimya hivi, JK (Jakaya Kikwete) alijenga UDOM bila kuwa kwenye Ilani ya CCM, JPM (John Magufuli) kajenga Bwawa la Stiglers, Ufufuaji ATCL, Kuhamia Dodoma, Daraja Kigongo/Busisi nk bila Ilani ya 2015/20,"inahoji sehemu ya andiko lake.

Nape ambaye aliwahi kufanya kazi pamoja na Mangula akiwa Katibu wa Itikadi na Uenezi na baada Waziri wa Habari kabla ya kuachwa, amehoji kulikuwa na kosa!Serikali kufanya jambo la masilahi kwa nchi na inafungwa na Ilani akamalizia kwa kusema 'Maajabu'.

Mradi wa Ujenzi wa bandari ya Bagamoyo uliasisiwa na Serikali ya awamu ya nne iliyoongozwa na Rais Jakaya Kikwete lakini Serikali ya awamu ya tano chini ya John Magufuli iliupinga.

Sababu za kuupinga zilielezwa ni kuwa mradi huo ungeliingiza Taifa katika hasara kubwa kutokana na masharti yaliyokuwa ndani yake.