Bei ya petroli, dizeli kupanda

Bei ya petroli, dizeli kupanda

Muktasari:

  • Bei ya mafuta kuanzia itapanda kuanzia kesho Septemba kwa sababu ilitajwa ni kutokana na soko la dunia.

Dodoma. Bei ya mafuta itapanda kuanzia Septemba Mosi sababu ikitajwa ni kutokana na soko la dunia.


Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura), Titus Kaguo amewaambia waandishi wa habari leo Jumanne Agosti 31, 2021 kuwa bei hizo zitaanza kutumika Septemba Mosi.

Kaguo ametaja bandari ya Dar es Salaam kuwa petroli imepanda kwa Sh84, dizeli Sh29 wakati mafuta ya taa bei ikiongezeka kwa Sh18.


"Bandari ya Tanga petroli imeongezeka kwa Sh53, dizeli Sh14 na mafuta ya taa yatabaki hivyo na bandari ya Mtwara petroli imeongezeka Sh108 na dizeli Sh46," amesema Kaguo.


Kwa mujibu wa meneja huyo, bei katika mikoa mingine itategemea na wanachukulia wapi mafuta hayo kati ya bandari hizo lakini bei ni elekezi.

Hata hivyo amesisitiza kama kuna mkoa ambao bei hazitaeleweka ama wenye mashaka, watume ujumbe mfupi wa maneno kuuliza bei hizo na watapokea majibu.