CCM yafuta matokeo ya uchaguzi Simiyu

CCM yafuta matokeo ya uchaguzi Simiyu

Muktasari:

Chama Cha Mapinduzi kimefuta matokeo ya uchaguzi wa Umoja wa Vijana (UVCCM) mkoa wa Simiyu kwa kilichodaiwa ni kuwepo kwa dalili wazi za rushwa.

Dodoma. Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimefuta matokeo ya uchaguzi wa Umoja wa Vijana (UVCCM) mkoa wa Simiyu kwa kilichodaiwa ni kuwepo kwa dalili za rushwa.


Mbali na Simiyu, lakini CCM kimesimamisha uchaguzi wa wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM kwa mikoa ya Arusha na Mbeya ambao wanatuhumiwa kutembeza rushwa huku wakionya uamuzi wa kufuta unaweza kuendelea katika maeneo yatakayobainika kukiuka sheria.

Kauli hiyo imetolewa leo Jumatatu Novemba 21,2022  na Katibu Mkuu wa CCM, Daniel Chongolo wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma.

Kwa mujibu wa Chongolo, leo ni siku ya tatu timu maalumu ya uchunguzi ipo huko ikichunguza zaidi kuhusu kilichojili ili vikao vifanye uamuzi.

Chongolo ametaja sababu kuu ni vitendo vya rushwa ambavyo vimetajwa katika maeneo hayo na kuwa chama hakitavulimia vitendo hivyo pale inapobainika.

"Mbali na hilo, tunachunguza kuhusu uchaguzi wa CCM mkoa wa Mjini Magharibi katika tuhuma za kada mmoja kubeba boksi la kura kwenda nalo chumba cha kuhesabia kura ikibainika tutatoa maelekezo ama ya kufuta matokeo au kuruhusu aliyetangazwa aendelee," amesema Chongolo.

Kiongozi huyo ambaye ni mkurugenzi wa uchaguzi ndani ya chama amesema hawako tayari kuona viongozi wanaingia madarakani kwa rushwa na vitendo viovu.

Kuhusu adhabu zitakazotolewa alisema ni kuondolewa kwenye mchakato wa uchaguzi na kupelekwa katika vyombo husika.