China yakaribisha wafanyabiashara kutoka Tanzania

China yakaribisha wafanyabiashara kutoka Tanzania

Muktasari:

  • Balozi wa Tanzania nchini China Mbelwa Kairuki ameikaribisha Kampuni ya China Silkroad Group kuwekeza nchini katika uongezaji wa thamani ya bidhaa za kilimo, samaki, nyama na madini

Dar es Salaam. Jumuiya za Biashara za Tanzania Bara na Zanzibar zimepewa fursa ya kufungua ofisi zao katika jengo jipya la biashara eneo Jiangbei New Area jijini Nanjing ili kuwezesha shughuli za biashara kati ya China na Tanzania.

 Fursa hiyo imetolewa jana na  Mwenyekiti wa China Silkroad Group Ndugu YAN Lijin wakati wa uzinduzi wa Jukwaa la Biashara kwa njia ya mtandao (DODR Silk Road Cross Border Duty Free & Digital Trade Centre).

 Jukwaa hilo lililozinduliwa jijini Nanjing katika Jimbo la Jiangsu, lilianzishwa na Kampuni ya China Silkroad Group na litatumika kuuza bidhaa za nje katika soko la China 

Katika hotuba ya ufunguzi wa jukwaa hilo, Mwenyekiti wa China Silkroad Group Ndugu YAN Lijin amesema  jukwaa hilo lina uwezo wa kuunganishwa na majukwaa ya biashara ya nchi za nje (E-commerce platforms) ili bidhaa za nje ziuzwe katika soko la China

Katika hafla hiyo, Balozi wa Tanzania nchini China Mbelwa Kairuki ameikaribisha Kampuni ya China Silkroad Group kuwekeza nchini katika uongezaji wa thamani ya bidhaa za kilimo, samaki, nyama na madini ili ziweze kuuzwa katika soko la China kupitia Jukwaa la Silk Road Cross Border Digitial Trade Centre.