DC Hanang' aagiza wavamizi msitu Gidamulod kuondoka
Mkuu wa Wilaya ya Hanang' Mkoani Manyara, Janeth Mayanja akizungumza baada ya kutembelea eneo la msitu wa Gidamulod. Picha na Joseph Lyimo
Muktasari:
Wavamizi hao wameanzisha mashamba kwenye msitu wa malisho katika Kata ya Dirma Wilaya ya Hanang' mkoani Manyara.
Hanang'. Mkuu wa Wilaya ya Hanang' mkoani Manyara, Janeth Mayanja ameagiza wavamizi wa msitu wa malisho wa Gidamulod katika Kijiji cha Qalosendo Kata ya Dirma kuondoka katika eneo hilo.
Mayanja akiwa na kamati ya usalama ya wilaya hiyo ametembelea eneo hilo na kuwaagiza wakulima waliovamia msitu huo kuondoka kwa kuwa eneo hilo ni kwaajili ya malisho ya mifugo.
"Wananchi wasio na nia njema wameanzisha mashamba kinyume na mpango ulioibuliwa mwaka 1996 na kurasimishwa mwaka 2008" amesema Mayanja.
Amewataka wavamizi hao waliojenga nyumba za muda maarufu tegesha kuondoka na watakaokaidi sheria itachukua mkondo wake.
Mwenyekiti wa kijiji cha Qalosendo, Gabriel Ng'yda amesema agizo hilo litakuwa na manufaa kwa uhifadhi wa msitu.