Dk Msuha: Tumejipanga kupunguza migongano ya binadamu, wanyamapori

Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Dk Maurus Msuha akizungumza akizungumza wakati wa kutambulisha mradi wa kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu katika kikao kilichofanyika jijini Dodoma
Muktasari:
- Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Dk Maurus Msuha amesema moja ya mkakati wa Wizara ya Maliasili na Utalii ni kuhakikisha migongano kati ya binadamu na wanyamapori hasa kwenye maeneo ya pembezoni mwa Hifadhi inapungua.
Dodoma. Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Dk Maurus Msuha amesema moja ya mkakati wa Wizara ya Maliasili na Utalii ni kuhakikisha migongano kati ya binadamu na wanyamapori hasa kwenye maeneo ya pembezoni mwa Hifadhi inapungua.
Dk Msuha ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Oktoba 18, 2022 wakati wa kutambulisha mradi wa kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu katika kikao kilichofanyika jijini Dodoma kilichozikutanisha timu ya wataalamu kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii na Shirika la Maendeleo ya Ujerumani (GIZ).
Hatua hiyo inakuja kufuatia Serikali ya Tanzania kupokea Euro milioni 6 sawa na Sh13.2 bilioni kutoka Shirika la Ujerumani la GIZ kwa ajili ya mradi wa kupunguza migogoro baina ya binadamu na wanyamapori katika mfumo wa Ikolojia Selous Niassa
Akizungumza katika kikao hicho, Dk Msuha amesema Serikali imekuwa ikifanya kila liwezekanalo ili kuhakikisha kuwa Wananchi wanaoishi karibu na maeneo ya Hifadhi hawaathiriwi na wanyamapori hao badala yake wanayatumia maeneo hayo katika kujinufaisha kiuchumi

Ameeleza kuwa moja ya mikakati ambayo Serikali imekuwa ikifanya ili kukabiliana na wanyamapori hao ni kuwavisha vifaa maalumu vya utambuzi kwa wanyamapori viongozi pamoja na kuwajengea uwezo wananchi katika kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu.
Mkurugenzi wa GIZ nchini Tanzania, Dk Mike Folke amesema Serikali ya Ujerumani imelazimika kutoa fedha hizo kutokana na jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali ya Tanzania katika Uhifadhi wa Wanyamapori
‘’Watanzania wanapenda sana uhifadhi wa wanyamapori hivyo kama migongano kati ya binadamu na wanyamapori hataidhibitiwa Watanzania hawa wanaowapenda wanyamapori wataanza kuuchukia uhifadhi ’’ amesistiza Dk Folke
Mradi huo wa kukabiliana na changamoto za wanyamapori wakali na waharibifu utakaofanyika baadhi ya Wilaya za Ruvuma zenye changamoto za wanyamapori unatarajiwa kuanza hivi karibuni na utadumu kwa kipindi cha muda wa miaka mitatu (2022-2025)