Faili la bosi TPA lakamilika, lasubiri CAG

Faili la bosi TPA lakamilika, lasubiri CAG

Muktasari:

  • Taasisi ya Kuzuia na Kupamabana na Rushwa (Takukuru) imesema imekamilisha faili la uchunguzi kuhusu tuhuma zinazomkabili aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Deusdedit Kakoko.

Dar es Salaam. Taasisi ya Kuzuia na Kupamabana na Rushwa (Takukuru) imesema imekamilisha faili la uchunguzi kuhusu tuhuma zinazomkabili aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Deusdedit Kakoko.

Machi 30, mwaka huu taasisi hiyo ilimkamata Kakoko ili kuhojiwa kuhusu tuhuma za ufisadi zilizomkabili ikiwa ni siku mbili baada ya Rais Samia Suluhu Hassan kuagiza asimamishwe ili kupisha uchunguzi kuhusu udokozi wa fedha za umma.

Rais Samia alimwagiza pia Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Dk Charles Kichere kuchunguza jinsi Sh bilioni 3.6 zilivyotumika kwenye mamlaka ya bandari.

Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Brigedia Jenerali John Mbungo amesema uchunguzi dhidhi ya bosi huyo na maofisa wengine umekamilika kwa asilimia 98.

“Asilimia mbili zilizobakia ni taarifa ya CAG ambayo ni muhimu sana, bila hiyo hatuwezi kwenda mahakamani.”

Mbungo alisema ripoti ya uchunguzi huo inahusisha pia sehemu ya taarifa ya CAG ili kudhibitisha tuhuma zinamkabili.