Gambo aibua tuhuma za kunusurika kuuawa mara mbili

Mbunge wa Arusha Mjini (CCM), Mrisho Gambo akisalimiana na wafanyabiashara wa eneo la soko kuu alipotembea kujua changamoto zao kabla ya kuelekea kwenye mkutano wa hadhara.

Muktasari:

  • Mbunge wa Arusha Mjini (CCM), Mrisho Gambo ameibua tuhuma dhidi ya viongozi wa Serikali akiwatuhumu kuuwinda uhai wake ikiwamo kumvamia nyumbani kwake eneo la Muriet kwa silaha mbalimbali.


Arusha. Mbunge wa Arusha Mjini (CCM), Mrisho Gambo ameibua tuhuma dhidi ya viongozi wa Serikali akiwatuhumu kuuwinda uhai wake ikiwamo kumvamia nyumbani kwake eneo la Muriet kwa silaha mbalimbali.

Hata hivyo, Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha, Justin Masejo amesema hana taarifa za mbunge huyo kuvamiwa

"Ofisini kwangu hakuna taarifa kama hiyo, ngoja nifuatilie kulingana na tuhuma alizotoa tuweze kulifanyia kazi," amesema Kamanda Masejo

Bila kuwataja viongozi hao anaowatuhumu, Gambo ametoa madai hayo jana Jumamosi Desemba 10, 2022 kwenye mkutano wa hadhara wa kusikiliza kero za wananchi eneo la soko kuu jijini Arusha iliyokwenda sambamba na kutoa msaada wa ujezi wa ofisi ya wafanyabiashara na mgawo wa gesi kwa mama ntilie.

Gambo ambaye amewahi kuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha alidai mbali na uvamizi wa nyumba yake pia viongozi hao ambao amewafahamu wamejaribu kumuua kwa sumu bila mafanikio.

"Yaani wameniwinda kuniua mara nyingi wameshindwa, wamevamia hadi nyumbani kwangu mara mbili lakini wamenikosa kwa sababu mimi mwenyewe ni mtoto wa mjini sio lofa," amedai Gambo na Kuongeza

"Wamejaribu kunitega na sumu pia wamenikosa kwa sababu kila ninapoenda naenda na maji yangu, sasa wanachoweza ni kunitega getini kwangu na kunipiga risasi," amedai mbunge huyo.

Amedai kuwa sababu kubwa ya kuwindwa hivyo ni kuibua tuhuma mbalimbali za ubadhirifu wa fedha za umma zinazofanywa na viongozi wa Serikali kitendo ambacho hawezi kukiacha.

"Yaani siwezi kuona ubadhirifu unaendelea halafu ninyamaze, ni bora niwe mbunge wa awamu moja lakini nimesema ukweli na hii ndio inanifanya naishi kwa hofu hii kwa sababu wanaoniwinda ni viongozi wa Serikali na nawatambua maana wako wanaonipigia simu eti nilitumwa nifanye hivyo," amedai

Akizungumza hilo, Diwani wa Muriet, Francis Mbise alisema mbunge huyo amevamiwa nyumbani kwake na watu walioshindwa kuwatambua.

"Ni kweli hizo taarifa alinipa na nazitambua lakini zaidi ya hapo sijui kama alichukua hatua gani," amesema Mbise

Tuhuma hizi za Gambo zimekuja akiwa na msuguano na baadhi ya viongozi wa CCM na Serikali tangu awatuhumu mbele za Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Mei 24 mwaka huu kuwa aliyekuwa Mkurugenzi Jiji la Arusha, Dk John Pima amekuwa ashirikiana na viongozi wengine kula fedha za Jiji.

Gambo ambaye alikuwa na orodha ya vigogo wa CCM akiwemo Katibu Mkuu wa UVCCM, Kenan Kihongosi na Serikali ambao walitumiwa miamala ya fedha alisema ni fedhea kuwataja wote hadharani.

Kutokana na tuhuma hizo za Gambo hadi sasa Dk Pima na maafisa wengine wajiji wanaendelea na kesi Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha.

Hata hivyo, Gambo kupitia mikutano yake ya hadhara amekuwa akiwataka baadhi ya viongozi wa chama tawala na Serikali kwenda Magereza kuwasalimia watuhumiwa hao na kuhoji dhamira zao.

Alisema ataendelea kukemea ufujajki fedha hata kama atakuwa mbunge wat emo moja.