Historia yaibeba UDSM Kongamano la Elimu

New Content Item (1)
New Content Item (1)

Muktasari:

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL), Bakari Machumu amesema wameamua kufanya kongamano la elimu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kutokana na historia yake.

Dar es Salaam. Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL), Bakari Machumu amesema wameamua kufanya kongamano la elimu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kutokana na historia yake.

Machumu ameyasema hayo leo Desemba 7, 2021 katika Kongamano la Sekta ya Elimu, kuelekea miaka 60 ya Uhuru lenye mada inayosema Ukuaji, Changamoto na mustakabali wa sekta hiyo.

Amesema lengo la kongamano hilo kutajadili changamoto na fursa zilizopo kuelekea miaka 60 ijayo. 

"Mnaweza mkadhani imetokea bahati mbaya kufanyia kongamano hili hapa, lakini ni makusudi kufanyia hapa kwasababu tunatambua jinsi ambavyo chuo hiki kina historia ndefu," amesema. 

Hata hivyo amebainisha kuwa walianza kampeni ya miaka ya 60 ya Uhuru Septemba 1, mwaka huu ambapo malengo yalikuwa kushiriki katika kukumbusha historia ya tulipotoka, mafanikio na tunapoelekea.

Amesema tayari yameshafanyika makongamano katika Sekta ya Nishati na Madini, Fedha, Miundombinu, Mashirika ya Kimataifa, Viwanda, Afya na Kilimo. 

"Tulichagua siku 100 na sasa leo ni siku ya 98 ambapo tunahitimisha kampeni yetu hii. Pamoja na makongamano haya pia tulikuwa tunatoa taarifa fupi fupi za kuikumbusha jamii tulipotoka," amesema Machumu.