Huduma ya WhatsApp bila simu janja yaja

Huduma ya WhatsApp bila simu janja yaja

Muktasari:

  • Huduma ya kutumiana ujumbe ya WhatsApp ambayo inamilikiwa na kampuni ya Facebook, inafanyiwa majaribio yatakayowezesha watumiaji kutohitaji simujanja.

San Francisco, Marekani (AFP). Huduma ya kutumiana ujumbe ya WhatsApp ambayo inamilikiwa na kampuni ya Facebook, inafanyiwa majaribio yatakayowezesha watumiaji kutohitaji simujanja.

Katika ujumbe uliotumwa katika blogu, wahandisi wa Facebook wamesema aina mpya itawezesha watumiaji wa huduma hiyo maarufu duniani, kuipata katika vifaa ambavyo si simu na bila kuhitaji kuunganisha na programu tumishi ya simu janja (smartphone app).

"Kwa kuwa na uwezo huu, sasa unaweza kutumia WhatsApp kwenye simu yako na hadi kwenye vifaa vingine vinne kwa wakati mmoja - hata kama betri ya simu yako imekufa," inasema taarifa hiyo.

Tangu ilipozinduliwa mwaka 2009, huduma hiyo ya kutumiana ujumbe kwa njia ya simujanja, imevuta watu bilioni mbili kote duniani na imenunuliwa na Facebook.

Kwa sasa WhatsApp inaweza kutumiwa kwa vifaa tofauti, kama vile kompyuta, lakini ikiunganishwa kwa njia ambayo kama simujanja ya mtumiaji haiko mtandaoni (offline) au betri imekwisha chaji, haiwezi kufanya kazi.

Mambo mengine yanaweza kuibuka kama kukatikatika kwa mara kwa mara.

"Teknolojia mpya ya kutumia WhatsApp kwa vifaa tofauti inaondoa "vikwazo hivi" kwa kutohitaji tena smartphone kufanya kila shughuli, kampuni hiyo imesema.

Kampuni hiyo pia iliwahakikishia wateja kuwa hatua za kiusalama za WhatsApp zitaendelea kufanya kazi chini ya mfumo mpya.

"Kila kifaa kitaunganishwa na WhatsApp bila kuingiliana huku tukiendeleza kiwango kile kile cha usiri na usalama ambao watu wanaotumia WhatsApp wamekuwa wakiutegemea."