IGP Wambura amalize mafaili hewa ya SIRRO

Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Camillius Wambura

Muktasari:

  • Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Camillius Wambura, tayari yupo ofisini. Amekalia kiti ambacho kinadaiwa mafaili mengi. Mtangulizi wake, Simon Sirro, hakuyapatia ufumbuzi.

Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Camillius Wambura, tayari yupo ofisini. Amekalia kiti ambacho kinadaiwa mafaili mengi. Mtangulizi wake, Simon Sirro, hakuyapatia ufumbuzi.

Mei 2017, wakati Sirro alipopokea kijiti cha u-IGP kutoka kwa Ernest Mangu, alikuta polisi kuna utata wa mtu aliyepotea bila maelezo yoyote. Anaitwa Ben Saanane. Mwanaharakati, kada wa Chadema na msaidizi binafsi wa Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.

Novemba 2016, Saanane alipotea. Haijulikani alipotelea wapi. Si Mangu wala Sirro waliweza kuwa na majibu au kama walikuwa nayo, hawakutoka kuuambia ukweli kuhusu kuhusu Saanane.

IGP Wambura ameingia. Novemba mwaka huu itatimia miaka sita tangu Saanane apotee. Pongezi kwa Wambura kuhusu cheo kipya ziende sanjari na kumkumbusha kuwa suala la Saanane bado tata. Ataweka alama akilishughulikia.

Kwa msamiati wa upelelezi wa makosa ya jinai, kesi kama ya Saanane huitwa “cold case” – “kesi baridi”. Kwa maana faili lake bado halijakamilika. Wambura ana wajibu wa kumaliza ‘ubaridi’ wa kesi ya Saanane.

Miezi miwili baada ya Sirro kuingia ofisini kama IGP akitokea kuwa Kamishna wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, aliyekuwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibondo, Simon Kanguye, alichukuliwa na watu wasiojulikana. Hadi leo hajarudi.

Huu ni mwaka tano tangu Kanguye atoweke. Hajulikani alipo. Haifahamiki ni akina nani walimchukua na kuondoka naye. Hili ni faili ambalo Sirro ameliacha wazi. Wambura ataweka heshima kubwa kama atalifanyia kazi na kila kitu kuwekwa hadharani.

Sirro akiwa anatimiza mwezi wa nne tangu aape kuwa IGP, aliyekuwa Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu, alishambuliwa kwa risasi takriban 38. Katika risasi hizo, 16 zilipenya na kuingia mwilini.

Lissu, alipigwa risasi mchana kweupe. Ndani ya uzio wa nyumba ambazo viongozi wa serikali na Bunge wanaishi. Wakati akishambuliwa, Lissu alikuwa Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani Bungeni.

Septemba 7, mwaka huu, itatimia miaka mitano tangu Lissu apigwe risasi. Polisi hawajawahi kutoka popote kueleza hali ya uchunguzi wa kesi ya Lissu. Ni cold case. Sirro ameacha bila majibu. Wambura atajenga heshima kubwa kama atalipatia majibu sakata hilo.

Miezi sita baada ya Sirro kushika usukani wa Jeshi la Polisi Tanzania, mwandishi wa habari wa Mwananchi Communications Ltd, Azory Gwanda, alichukuliwa na watu wasiojulikana. Novemba mwaka huu itatimia miaka mitano tangu Azory atoweke.

Utata ni mkubwa kuhusu Azory aliyekuwa mstari wa mbele kufuatilia matukio ya mauaji Kibiti. Polisi hawajawahi kutoa kauli yenye uzito kuhusu kupotea kwa Azory. Watanzania na jumuiya ya wanahabari watampa thamani kubwa Wambura kama atalishughulia faili la Azory ambalo limeachwa wazi na Sirro.

Kuanzia mwaka 2017 mpaka 2018, taifa lilitikiswa na habari za matukio ya maiti kuokotwa kwenye fukwe za Bahari ya Hindi na Mto Ruvu, zikiwa zimefungwa mithili ya vifurushi.

Waziri wa Mambo ya Ndani wakati huo, Mwigulu Nchemba, alipata kutoa maijibu kuwa maiti zilizokutwa Mto Ruvu ni waathirika wa biashara haramu ya binadamu (human trafficking). Maelezo ya ufafanuzi wa ripoti hiyo yalikosekana.

Mpaka leo polisi hawajawahi kueleza ni kitu gani kilitokea mpaka watu wengi walipoteza maisha kwa mtindo unaofanana. Jinsi maiti zilivyokutwa zimefungwa kwenye mifuko ya sandarusi inalaribisha dhana ya karibu kuwa waliuawa.

Je, ni akina nani hao? Walifanya nini? Waliohusika na mauji walipatikana? Walichukuliwa hatua gani? Bado wanatafutwa? Wananchi wanahitaji majibu. Wambura anapaswa kuja na majibu mengi kuhusu matukio yaliyoachwa njiapanda kipindi cha uongozi wa Sirro.

Kuna madhila mengi yalitokea wakati wa uongozi wa Sirro. Watu kukamatwa kama mateka, baada ya kekele nyingi za vyombo vya habari na mitandao ya kijamii ndipo iliripotiwa kuwa wahusika walikuwa vituoni.

Haya ni mambo ambayo Wambura bila shaka anayajua kikamilifu. Wakati Sirro anakuwa IGP, yeye alikuwa Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalum Dar es Salaam, kuna kipindi alikuwa Kamanda wa Polisi Manyara. Nyakati za mwisho za u-IGP wa Sirro, Wambura alikuwa Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI).

Analijua vizuri jeshi, mapito, mafanikio na changamoto zake. Hivyo, anayo nafasi ya kusahihisha makosa ambayo mtangulizi wake aliyafanya. Miaka mitano ya Sirro, Jeshi la Polisi Tanzania lililaumiwa kuliko kusifiwa.

Sinema ya kutekwa mfanyabiashara Mohammed Dewji ‘MO’, hadi leo hakuna ambaye ameuelewa mwendelezo na mwisho wake. Wengi wanaamini kuwa kuna jambo linafichwa. Rais wa Tano wa Tanzania, Dk John Magufuli, alipata kumwambia Sirro kuhusu kutekwa kwa MO: “Msidhani Watanzania ni wajinga.”

Wambura anaweza kuichukua kauli ya Magufuli kuwa “Watanzania sio wajinga”, kisha yeye asaidie kupata majibu ambayo yatamfanya akiondoka akumbukwe. Na iliwezekana mrithi wake apate wakati mgumu kuvaa viatu vyake.

Kwa Wambura imekuwa rahisi kuvaa viatu vya Sirro, maana katika uongozi wake wa miaka mitano ameacha viulizo vingi kuliko ufumbuzi wa mambo ya msingi yaliyolizonga taifa.

Kipindi cha Sirro ndipo ilibainika kuwa watu wengi wasio na hatia walibambikiwa kesi. Ushahidi wa hili ni tamko la Rais Samia Suluhu Hassan, kuwa baada ya kuingia ofisini kesi nyingi za kubambikia watu zilifutwa, kuanzia polisi hadi Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).

Unaweza pia kurejea ripoti ya mwaka 2019 ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Buswalo Mganga, kuwa polisi Tabora waliwabambikia wananchi wawili kesi ya mauaji, wakati wakijua ni uongo.


Wambura ajenge jeshi gani?

Swali hili, kwangu litakuwa na majibu mengi. Hata hivyo, la kwanza kabisa ni Wambura kuamua kwa dhati kabisa kuwa kiongozi wa tofauti na mtangulizi wake. Asimuige Sirro hata kidogo.

Anachotakiwa kufanya ni kujenga jeshi lenye kulinda raia. Ataweka alama kama atafanikiwa kulifanya Jeshi la Polisi liwe na sura halisi ya kijeshi na sio kutumika kisiasa kwa masilahi ya wanasiasa. Sirro alilifanya Jeshi la Polisi Tanzania kuwa kama mali ya wanasiasa.

Kesi zichunguzwe na zifike mwisho. Wakosaji ndani ya polisi wachukuliwe hatua. Mwaka 2017, mtu anayedaiwa kuwa askari polisi, alimtolea bastola Waziri wa Habari na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, Nape Nnauye. Kipindi hicho, Nape alikuwa ametenguliwa uwaziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Mtu huyo hakukamatwa wala kufunguliwa mashitaka. Je alikuwa polisi? Alitumwa na nani kwenda kumshughulikia Nape? Kosa la Nape lilikuwa nini? Nape alikwenda kuzungumza na waandishi wa habari Hoteli ya Protea, Oysterbay, Dar es Salaam.

Wambura anatakiwa kujenga jeshi la kistaarabu. Lisilo na upendeleo kwa raia. Rushwa isiwe nyenzo ya kupata haki. Tajiri na maskini wapewe huduma sawa. Aliondoe jeshi la polisi kwenye kasumba ya maofisa wake kugeuka chawa (wapambe) wa matajiri wahalifu. Matokeo yake uhalifu unaendelea.

Polisi hapaswi kuwa chawa ili aitende kazi yake inavyotakiwa.


Sasa hivi si shwari. Polisi wanashinda kwenye makwapa ya wahalifu wenye fedha. Kuna ambao wanapokea mishahara kutoka kwa wahalifu ili wawalinde. Haya yapo. Wambura bila shaka anayajua kwa sababu amehudumia jeshi mjini. Ayaondoe haya. Jeshi liwe na meno. Kibebe hadhi inayostahili.

Natamani pia kipindi cha Wambura wanawake ndani ya Jeshi la Polisi wawezeshwe zaidi na wapae. Wasididimizwe. Tuwe na makamishna wengi wanawake.

Tusichelewe sana kuona nchi inakuwa na DCI mwanamke. Au akiondoka Wambura impendeze Rais kumteua IGP mwanamke. Inawezekana!

atilie migogoro ndani ya vyama na baina ya vyama na serikali, mfano mpira wa miguu umeweka taratibu zake kwenye masuala ya soka, huo ni mfano mmojawapo mzuri.

Ushauri huu ulikataliwa, lakini naamini mpaka sasa hilo ndilo suluhisho.

Mbali na chombo hicho, kila chama kinapaswa kuwa na mbinu na mikakati ya kukabiliana na migogoro. Kwanza kuwa na Katiba imara inayokubalika na kanuni zinazoeleweka na kuwa na mbinu na rasilimali watu wenye weledi katika kutatua migogoro ndani ya chama.

Swali: Katika harakati zako ulishiriki katika mchakato wa Katiba, ambao baadhi ya vyama vilisusia Bunge Maalumu la Katiba na mpaka leo Katiba haijapatikana. Unauonaje huu mchakato kwa sasa?

Jibu: Siku zote mlevi hasusiwi pombe, kwa sababu ukisusa, atafunga shati kiuononi na ataimaliza pombe.

Tabia ya kususa haikuanza tu kwenye uchaguzi wa Zanzibar, bali imekuwepo hata kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano ambapo vyama vyetu vimekuwa vikisusa kwa sababu hii au ile, ingawa uchache wetu pia kwenye vyombo vya maamuzi mara nyingi umetufanya tuone kuwa hii ni njia muhimu, japo kwa mtazamo wangu naona kususa ni dalili ya woga.

Hapa historia inatuonesha mara zote tukisusa, wenzetu wanasonga mbele na kwahiyo kama tulikuwa na hoja ya msingi inafifia kama siyo kufa kabisa, tabia hii siyo nzuri, tunalijeruhi taifa letu.

Tumesusa Bunge la Katiba, tunaunda Ukawa (Umoja wa katiba. Mimi nilikuwa miongoni mwa viongozi wanane walioanzisha Ukawa, lakini baadaye kukawa na ubaguzi, sisi ambao vyama vyetu havikuwa na wabunge tukabaguliwa.

Tukaambiwa tunaishi kwa fadhila ya kuteuliwa na Rais na tunataka Bunge liendelee. Nikawauliza, kwani tuko hapa kwa ajili ya nini? Si kwa ajili ya Katiba?

Kwenye majadiliano kama haya kuna kupokea na kupoteza, naamini kuna mambo katika Bunge lile tungeyasimamia kidete tungepata mwelekeo mzuri sana kama taifa, lakini kususa kumetunyima kila kitu hadi tume huru ya uchaguzi, chombo ambacho ni muhimu sana katika kuipima demokrasia yetu.

Jambo la pili ni kwamba katika mchakato ule, kipimo cha mwisho ni kura ya mwananchi. Naamini kama tungebaki kwenye bunge lile tukapigania walichosema wananchi, halafu mwisho wa siku kikakataliwa na walio wengi, basi mwisho wa siku tungekuwa na uhalali wa kwenda kwa wananchi na kuwaeleza juu ya kilichopendekezwa na kile kilichopitishwa.