JK amsotesha mkurugenzi wa Sumatra mbele ya madereva

Rais Jakaya Kikwete, akizungumza na madereva katika mkutano uliondaliwa na Chama Cha Wafanyakazi Madereva Tanzania (TADWU), uliofanyika Dar es Salaam jana. Picha na Ikulu

Muktasari:

Rais alifanya hivyo baada ya kusikiliza risala iliyosomwa na kaimu katibu wa Chama cha Madereva wa Vyombo vya Moto, (TADRWU), Rashid Salehe iliyoeleza kuwa wamemuita kuwasikiliza kutokana na kutopatikana ufumbuzi wa madai yao, likiwamo la mikataba ya ajira na kusafiri bila posho ya safari, huku akiishutumu Sumatra kuwapa stika wamiliki wa magari bila kuwa na mikataba ya wafanyakazi wao kama walivyokubaliana.

Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete jana alimpa wakati mgumu mkurugenzi wa Mamlaka ya Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra), Giliadi Ngewe baada ya kumtaka aeleze sababu zinazomkwamisha kutatua na kuhakiki mikataba ya madereva.

Rais alifanya hivyo baada ya kusikiliza risala iliyosomwa na kaimu katibu wa Chama cha Madereva wa Vyombo vya Moto, (TADRWU), Rashid Salehe iliyoeleza kuwa wamemuita kuwasikiliza kutokana na kutopatikana ufumbuzi wa madai yao, likiwamo la mikataba ya ajira na kusafiri bila posho ya safari, huku akiishutumu Sumatra kuwapa stika wamiliki wa magari bila kuwa na mikataba ya wafanyakazi wao kama walivyokubaliana.

Rais Kikwete alikutana na madereva wa vyombo vya moto wa jijini Dar es Salaam waliokuwa wamemuomba asikilize madai yao mbalimbali.

Mbele ya madereva hao, Rais Kikwete alimuita mkurugenzi huyo ili atoe maelezo, na Ngewe alisema tayari ana mikataba ya madereva 6,000 kwa ajili ya kuifanyia uhakiki kutoka kwa wamiliki wa magari, na baada ya kauli hiyo madereva walimzomea na kusema si kweli.

Mkurugenzi huyo alitakiwa kueleza walianza lini uhakiki kama walivyokubaliana na wawakilishi wa madereva, ndipo alipojibu kuwa ilikuwa waanze Oktoba Mosi.

Rais Kikwete alimuuliza lini, lakini akaeleza kuwa wataanza baada ya kukaa na maofisa wa Wizara ya Kazi na Ajira.

Rais hakuridhika na majibu hayo na kumtaka aeleze siku ambayo ataanza kuhakiki mikataba hiyo kwa kuhusisha viongozi wa vyama vyote vya madereva.

Ngewe alimwambia Rais Kikwete atafanya hivyo baada ya mkutano huo.

Hata hivyo, Rais Kikwete alitumia mkutano huo kuwananga Sumatra kwa kushindwa kusimamia makubaliano na madereva hao, ikiwa ni pamoja na kupinga wazo lao la kutaka wakaguliwe mikataba kwenye mizani.

Alimlaumu Mkurugenzi huyo kukataa njia hiyo rahisi na badala yake kufanya tofauti na walivyokubaliana kitu kinachozidisha hasira za madereva, “Nielezeni mtakachokubaliana Jumatatu, nitatoka kidogo siendi mbali Jumanne nitakuwa nimerudi, ”alisema Kikwete na kushangiliwa na madereva hao.

Huku akishangiliwa kila anapopita au kutajwa licha ya kuzungumza Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Mkonda alitumia mkutano huo kuwaombea vifaa vya ofisi madereva hao, ambapo Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Saidi Meck Sadiq aliahidi kuwanunulia kompyuta na rais kuahidi kuwapa Sh100 milioni kusimamisha umoja huo.