Kada wa CCM aachiwa huru

Muktasari:

Uamuzi huo ulitolewa na Hakimu Mkazi Mkuu, Respicius Mwijage baada ya Mwendesha Mashtaka wa Bodi ya Usajili wa Makandarasi (ERB), Saddy Kambona kuomba kesi hiyo iondolewe mahakamani hapo chini ya kifungu cha 98 (a) cha sheria ya Makosa ya Jinai (CPA).

Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu  imemuachia huru Kada wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Thomas Ngawaiya aliyekuwa akikabiliwa na shtaka la kujenga hoteli kwa kutumia makandarasi wasiosajiliwa.

Uamuzi huo ulitolewa na Hakimu Mkazi Mkuu, Respicius Mwijage baada ya Mwendesha Mashtaka wa Bodi ya Usajili wa Makandarasi (ERB), Saddy Kambona kuomba kesi hiyo iondolewe mahakamani hapo chini ya kifungu cha 98 (a) cha sheria ya Makosa ya Jinai (CPA).

Baada ya kutolewa kwa ombi hilo, Hakimu Mwijage alikubaliana nalo na kumuachia huru Ngawaiya.

Awali, Kambona alidai kuwa, Ngawaiya ambaye aliwahi kuwa Mbunge wa Moshi vijijini na pia Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi mkoa wa Kilimanjaro alifikishwa mahakamani hapo kwa kukaidi amri ya mahakama, akasomewa shtaka hilo na kulikana.

Ngawaiya alidaiwa kuwa Machi 24,2015 nyakati za mchana alitenda kosa hilo kwa  kuagiza ujenzi wa jengo la hoteli kwa watu ambao hawajasajiliwa na bodi ya Usajili wa Makandarasi.

 Jengo hilo lipo kwenye kiwanja namba 32 kilichopo makutano ya mtaa wa Dosi na Wazani eneo la Magomeni Mapipa Wilaya ya Kinondoni jijini D ar es Salaam.

Mshtakiwa huyo anadaiwa kutenda kosa hilo kinyume na kifungu namba 22 cha sheria ya bodi ya Usajil wa Makandarasi  namba 17,ya mwaka 1997.

Saddy alidai kuwa sheria hiyo inamtaka kila anayejenga jengo ambalo ni kwa matumizi ya umma lazima atumie makandarasi waliosajiliwa na ERB.