Kamati bei ya mafuta yakabidhi ripoti kwa Waziri Mkuu

Muktasari:

  •  Serikali ya Tanzania imesema kamati iliyoundwa kuchunguza kupanda kwa bei ya mafuta imewasilisha ripoti yake kwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.


Morogoro. Serikali ya Tanzania imesema kamati iliyoundwa kuchunguza kupanda kwa bei ya mafuta imewasilisha ripoti yake kwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.

Akizungumza na vyombo vya habari leo Jumamosi Oktoba 2, 2021 Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amesema Waziri Mkuu ameshapokea ripoti hiyo.

“Serikali kupitia kwa Waziri Mkuu (Kassim Majaliwa) Ilisitisha bei mpya zilizotangazwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (Ewura) mpaka zitathiminiwe kwanza yale maeneo yote yanayotengeza bei ya bidhaa ya mafuta” amesema Msigwa.

“Kamati ile iliyokuwa imeundwa na Waziri Mkuu imeshakamilisha kazi yake imekabidhi ripoti juzi na Waziri Mkuu ameikabidhi kwa Waziri wa Nishati (January Makamba) na yeye anaifanyia kazi na wakati wowote Serikali itakuja kuwaambia uamuzi wake juu ya eneo hili.”Amesema Msigwa.

Kamati hiyo iliundwa Septemba 2, 2021 na ilipewa wiki mbili kukamilisha kazi ya kuchunguza kupanda kwa bei ya mafuta.