Kesi ya kina Mdee kuanza leo mchana

Muktasari:

  • Shauri la waliokuwa wanachama 19 wa Chadema, Halima Mdee na wenzake wanaoomba ridhaa ya mahakama kufungua shauri la kupinga uamuzi wa chama chao kuwavua uanachama linaanza leo Jumatatu, Juni 27, 2022 mchana.


Dar es Salaam. Shauri la waliokuwa wanachama 19 wa Chadema, Halima Mdee na wenzake wanaoomba ridhaa ya mahakama kufungua shauri la kupinga uamuzi wa chama chao kuwavua uanachama linaanza leo Jumatatu, Juni 27, mwaka huu mchana.

Mdee na wenzake 18 walifungua maombi hayo Mahakama Kuu Masjala Kuu dhidi ya Chadema, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Alhamisi Juni 23, mwaka huu.

Hii ni mara ya pili Mdee na wenzake kufungua maombi hayo baada ya maombi yao ya awali kutupwa na mahakama hiyo, kutokana na kasoro za kisheria.

Kiongozi wa jopo mawakili wa kina Mdee, Aliko Mwamanenge, ameliambia Mwanachi kuwa shauri hilo limepangwa kuanza kutajwa leo mchana na kwamba limepangwa kusikilizwa na Jaji Mustapha Ismail.

“Shauri limepangwa kwa ajili ya mention (Kutajwa) leo saa nane mchana lakini pia tutaomba tusikilizwe na maombi yetu ya ku-maintain satatus quo (kudumisha hali iliyopo yaani kulinda hadhi ya ubunge wa kina Mdee), kama mazingira yataruhusu.”, alisema Mwamanenge.