Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

KESI YA UKAHABA: Shahidi Polisi alivyobanwa na mawakili kuhusu maana ya ‘umalaya’

Washtakiwa wanaodaiwa kuwa makahaba wakiwa kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Sokoine Drive (Jiji). Picha na Pamela Chilongola

Muktasari:

  • Shahidi ameieleza mahakama kuwa viashiria vya ukahaba vilivyofanya wakawakamta watuhumiwa ni mavazi na muda lakini alijikuta katika wakati mgumu kujibu maswali kuhusu maana ya ukahaba.

Dar es Salaam. Shahidi wa pili katika kesi ya ukahaba inayowakabili washtakiwa watano katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Sokoine Drive, ameileza mahakama hiyo kuwa waliwakamata washtakiwa hao kwa tuhuma za ukahaba kutokana na viashiria vya aina ya mavazi waliyokuwa wameyavaa na muda na mahali walikokutwa na polisi.

Hata hivyo, shahidi huyo ambaye ni askari kutoka Kituo cha Polisi Mburahati, WP  Konstebo wa Polisi (PC), Tunusuru Malungula, alijikuta katika wakati mgumu alipotakiwa kueleza maana ya umalaya au ukahaba kutokana na viashiria hivyo alivyovitaja.

Ilikuwa ni wakati wa maswali ya dodoso aliyoulizwa na mawakili wa utetezi katika kesi hiyo, Peter Madeleka, Jebra Kambole na Maria Mushi, leo Alhamisi Juni 27, 2024, mpaka akasema kuwa hajui maana ya ukahaba.

Pia, amesema hajui kama kuna sheria inayobainisha sifa za mavazi yanayoashiria ukahaba wala inayoweka muda ambao mtu akikutwa barabarani anakuwa anajihusisha na ukahaba.

Shahidi huyo pia alitakiwa kueleza kama washtakiwa walikuwa wakiuza miili yao, wao walibaki na nini na wateja walioinunua wako wapi.

Washtakiwa katika kesi hiyo inayosikilizwa na Hakimu Mfawidhi Rachael Kasebele ni Mariam Yusufu Mkinde (25) mkazi wa Magomeni, Mwazani Nassoro (25) mkazi wa Kigogo, Mwanaidi Salum (25) mkazi wa Mabibo, Faudhia Hassan (35) mkazi wa Ubungo na Tatu Omary (40) mkazi wa Ubungo.

Katika kesi hiyo ya jinai namba 17277/2024, washtakiwa hao wanakabiliwa na shtaka moja la kufanya vitendo vya aibu mbele ya hadhara kwa ajili ya kufanya umalaya, kinyume na kifungu cha 176 (a) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16, marejeo ya mwaka 2022.

Wanadaiwa kuwa Juni 17, eneo la Manzese Tip Top, Wilayani Ubungo, Dar es Salaam, walikutwa wakifanya vitendo vya aibu mbele ya hadhara kwa kusimama hadharani, wakiwa wamevaa mavazi yasiyo ya heshima kwa lengo la kufanya umalaya.

Awali, katika ushahidi wake wa msingi akiongozwa na waendesha mashtaka wawili kwa zamu, Mawakili wa Serikali Winfrida Ouko na Tumaini Mafuru, PC Tunusuru alieleza kuwa washtaakiwa polisi liwakamata washtakiwa hao Juni 17, 2024, wakati wakiwa katika doria yeye na wenzake watano.

PC Tunusuru ameieleza mahakama kuwa waliwakamata muda wa saa tisa usiku eneo la Manzese Tip Top, Mtaa wa Midizini, ambapo waliwaona vema kwa kuwa walikuwa wamesimama eneo la biashara palipokuwa na mwanga na kwamba kilichofanya wakawakamata ni viashiria vya ukahaba.

Amevitaja viashiria hivyo kuwa ni aina ya mavazi yasiyo ya heshima waliyokuwa wamevaa, muda na kitendo cha kuanza kukimbia baada ya kuwaona askari.

“Mfano, Mwadhani alikuwa amevaa nguo aina ya tight nyepesi sana ambayo ilikuwa imemchora maumbile,” ameeleza shahidi huyo na kuwa walipowahoji kwa nini wanafanya hivyo, kila mmoja alitoa sababu zake na wengine wakidai hawapendi bali ni kwa sababu wanategemewa.

Shahidi huyo amewatambua mahakamani huku akiieleza mahakama kuwa amefanikiwa kuwatambua kwa kuwa alikutana nao muda mrefu, kwani baada ya kuwakamata waliwapeleka Kituo cha Polisi Mburahati na kuendelea na taratibu nyingine za kuchukua taarifa zao.

Baada ya maelezo hayo, ndipo shahidi huyo akaulizwa maswali kutoka kwa mawakili wa utetezi, kuhusu ushahidi wake.

Maswali ya dodoso

Wakili Madeleka: Shahidi hebu ikumbushe Mahakama dini yako, umesema ni dini gani?

Shahidi: Muislamu

Wakili: Kwa sababu wewe ni Muislam umeapa kwa Kuran na unaiamini, hebu ieleze Mahakama Surat Yasin (Sura ya Sita) inasemaje?

Shahidi: Sijui

Wakili: Umesema wewe ni askari polisi, ni sahihi?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Askari polisi anatambulika kwa sare na kitambulisho cha kazi ni sahihi?

Shahidi: Ni kweli

Wakili: Na kwamba nje ya hizo njia mbili haiwezekani kumtambua askari?

Shahidi: Si sahihi

Wakili: Jeshi la Polisi huwa linatoa vitambulisho kwa askari wake, ni sahihi?

Wakili: Wewe hapa umevaa sare za polisi?

Shahidi: Sijavaa

Wakili: Umemwonyesha mheshimiwa hakimu kitambulisho?

Shahidi: Sijamwonyesha.

Wakili: Shahidi, mheshimiwa hakimu mnafahamiana?

Shahidi: Hapana.

Wakili: Kwa hiyo ukimwambia tu kuwa wewe ni polisi kwa hivyo ulivyo, atakuamini?

Shahidi: Hawezi kuamini

Wakili: Umemwambia mheshimiwa hakimu kwamba washtakiwa hawa walikamatwa na polisi waliokuwa doria ukiwemo wewe, ni sahihi?

Shahidi: Ni sahihi.

Wakili: Kwa kuwa umesema kwa hivyo ulivyo ni vigumu mheshimiwa hakimu kukuamini kuwa wewe ni askari, je unataka Mahakama isiamini kuwa wewe ulishiriki kuwakamata hawa washtakiwa?

Shahidi: Hapana

Wakili: Ulisema ulikwenda kuwakamata mkiwa askari sita na umewataja Afande Peter,  Jackson Masali na ..., ni sahihi kwamba hakuna askari polisi mwenye jina moja, ila mawili au matatu waliyotumia katika kuwaajiri?

Shahidi: Ni sahihi.

Wakili: Ni sahihi kwamba kwenye Jeshi la Polisi kuna askari wengi wanaitwa Peter?

Shahidi: Ni sahihi.

Wakili: Sasa hawa askari wewe uliowataja kwa jina moja ni askari polisi ambao kweli wana majina mawili au matatu kama ulivyosema?

Shahidi: Ni askari.

Wakili: Wewe binafsi ulishiriki kumkamata nani kati ya hawa?

Shahidi: Mwazani

Wakili: Unakumbuka hawa wengine waliobaki walikamatwa na nani?

Shahidi: Sikumbuki

Wakili: Unakubaliana na mimi kwa mujibu wa sheria za Polisi mtuhumiwa mwanamke anapaswa kukamatwa na askari mwanamke?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Na mwanamke akikamatwa na askari mwanaume ni udhalilishaji, si ndiyo?

Shahidi: Ndiyo.

Wakili: Na timu ya ukamataji askari, wanawake walikuwa wawili tu, si ndiyo?

Shahidi: Ndiyo.

Wakili: Kwa kuwa wewe ulimkamata mmoja tu, Mwazani, mwambie mheshimiwa hakimu, hawa wengine walikamatwa na nani?

Shahidi: Walikamatwa na wale askari wengine akiwemo na Masaji (mwanamke), walikamatwa na Masali

Wakili: Umesema viashiria vya ukahaba ni kwamba baadhi walipowaona walianza kukimbia na umesema wengine wote walikamatwa na Masali, ina maana Masali alikuwa anawakimbiza mmoja mmoja, anamkamata anamleta huku wengine wanaendelea kukimbia, kisha anawakimbilia na kuwakamata?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Mlikuwa na warrant of arrest (kibali cha ukamataji)?

Shahidi: Tulikuwa nayo.

Wakili: Wakati ukiongozwa na wakili wa Serikali (kutoa ushahidi) ulimwambia mheshimiwa hakimu kuwa ukamataji huo mlifanya kwa warrant of arrest?

Shahidi: Sikuwambia.

Wakili: Kwa hiyo warrant ilikuwa na majina ya watuhumiwa?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Hiyo warrant umeiona hapa mahakamani?

Shahidi: Hapana

Wakili: Ulimwambia mheshimiwa hakimu kuhusu hiyo RB?

Shahidi: Sikumwambia

Wakili: Mtuhumiwa akikamatwa akifikishwa Polisi huwa anandika maelezo, na waliomkamata huwa wanashiriki kuandika maelezo yao, uliandika maelezo ya hao watuhumiwa?

Shahidi: Hapana

Wakili: Wewe uliandika maelezo yako kama mkamataji?

Shahidi: Sikuandika

Wakili: Sasa kama hukuandika wewe hujavunja Sheria?

Shahidi: Hapana

Wakili: Umesema viashiria vya kwamba walikuwa ni makahaba vilikuwa nini na nini?

Shahidi: Mavazi na muda

Wakili: Kwa hiyo viashiria vya umalaya ni mavazi na muda, sawa?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Kuhusu kiashiria cha mavazi ulisema ni mmoja tu aliyekuwa amevaa kitopu, kwa hiyo hao wengine uliwaonea (kuwakamata)?

Shahidi: Hapana

Wakili: Hicho kitop umekiona hapa mahakamani, yaani hapa mahakamani hicho kitopu kipo?

Shahidi: Hakipo

Wakili: Kwa hiyo hilo la kitop ni hadithi zako tu?

Shahidi: Hapana sio hadithi zangu.

Wakili: Umesema moja ya majukumu yako ni kulinda sheria, na bila shaka unazijua hizo sheria?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Hebu ieleze mahakama ni sheria gani inasema kuvaa kitop ni umalaya?

Shahidi: Sijui.

Wakili: Umesema vazi lingine ni tight (taiti) nyepesi, umeileta hapa mahakamani?

Shahidi: Hapana.

Wakili: Askari anapotoka kwenda kwenye operesheni huwa anaandika majina yake kwenye OB (kitabu cha matukio), ni sahihi?

Shahidi: Ni sahihi.

Wakili: Wewe uliandika majina yako kwenye OB?

Shahidi: Sikumbuki

Wakili: OB ni moja ya vitendea kazi vyako muhimu, ni sahihi?

Shahidi: Ndiyo.

Wakili: Unawezaje kusahau kitendea kazi chako muhimu, ambacho unakitumia kila siku lakini ukakumbuka majina ya washtakiwa na vitopu, huoni wewe ni muongo?

Shahidi:  Sio muongo.

Wakili:  Mlipotoka nao huko mlikowakamata na mkawapitisha CRO (chumba cha mashtaka Kituo cha Polisi) mlikowakabidhisha, mliwakabidhisha kwa utaratibu gani?

Shahidi: Sikumbuki.

Wakili: Pia hukumbuki kama waliandikishwa katika OB?

Shahidi: Waliandikishwa.

Wakili: OB namba ngapi?

Shahidi: Sikumbuki

Wakili: Hiyo OB umeileta hapa mahakamani?

Shahidi: Hapana.

Wakili Kambole: Shahidi wewe hukumkamata Mariam (mshtakiwa wa kwanza) ni, sahihi?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Kwa hiyo hujui Mariam alivaa nguo gani?

Shahidi: Sijui.

Wakili:  Umesema mlikuwa na arrest warrant, ilikuwa na majina haikuwa na majina?

Shahidi: Sikumbuki

Wakili: Shahidi unaweza kutusaidia hapa mahakamani umalaya maana yake ni nini?

Shahidi: Sijui

Hakimu: Hujui maana ya umalaya?

Shahidi: Ni kujihusisha na ukahaba

Wakili: Ukahaba ni nini?

Shahidi: Ni moja ya viashiria vya umalaya.

Wakili: Kwa hiyo ukahaba ni moja ya viashiria vya umalaya na umalaya ni nini?

Shahidi: Ni vitendo vya kujihusisha na ukahaba.

Wakili: Kwa mujibu wa sheria gani?

Shahidi: Sijui.

Wakili: Kwa hiyo wewe ulikuwa unatekeleza sheria ambayo wewe huijui?

Shahidi: Hapana, sababu sheria inakataza vitendo vya umalaya

Wakili: Sheria gani?

Shahidi: Sikumbuki.

Wakili: Shahidi, umesema kiashiria kingine cha kuwakamata kwa ukahaba ni muda, kwani ni kuanzia saa ngapi mtu akitembea barabarani anakuwa anafanya umalaya?

Shahidi: Sijui

Wakili: Kwa kuwa hujui, utakubaliana na mimi kwamba muda si kiashiria cha umalaya?

Shahidi: Sitaweza kukubaliana na wewe

Wakili: Haya mwambie Mheshimiwa ni kuanzia saa ngapi?

Shahidi: Nimeshasema sijui.

Wakili: Hawa washtakiwa walikamatwa saa ngapi?

Shahidi: Saa 9 usiku.

Wakili: Wewe unajua walikuwa wanakwenda au wanatoka wapi?

Shahidi: Sijui

Wakili: Utakubaliana na mimi kuwa wakati unaongozwa na wakili wa Serikali hukusema kama walikuwa wamesimama na mwanaume au hawakuwa wamesimama na wanaume?

Shahidi: Sijaulizwa, sikuwaona.

Wakili: Wakati unatoa maelezo yako ulisema baada ya kuwakamata mliwauliza kwa nini wanafanya hivyo, mwingine akasema anategemewa na mwingine kwamba sio kupenda kwake, hayo maelezo kuna sehemu uliyaandika?

Shahidi: Sikuyaandika

Wakili: Kwa hiyo hakuna ushahidi huo?

Shahidi: Ushahidi upo

Wakili: Uko wapi?

Shahidi: Sikuyaandika

Wakili: Utakubaliana na mimi kuvaa vitopu si kosa la jinai?

Shahidi: Ni kosa maana si nguo za heshima

Wakili: Kwa mujibu wako nguo za heshima ni zipi?

Shahidi: Zinazofunika maumbile

Wakili: Ambayo ni yapi?

Shahidi: Nguo ndefu

Wakili: Kuna Sheria inayotoa mwongozo wa mavazi?

Shahidi: Sijui

Wakili: Hilo unalolisema ni kwa mujibu wa nini?

Shahidi: Sijui

Wakili: Shahidi, ni sahihi kwamba hawa washtakiwa hata kama uliwakamata ni kwa mara ya kwanza ndio uliwaona ulipowakamata?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Utakubaliana na mimi kwamba hujui pale walikuwa wamekaa kwa muda gani?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Shahidi kwa mara ya kwanza umesema uliwaona saa tisa na hujui walikuwa wamekaa kwa muda gani, na kama walikuwa wanapita au?

Shahidi: Sikumbuki

Wakili: Walikaa kwa muda gani pale?

Shahidi: Sijui

Wakili: Lakini pia wewe hujui ni nini hasa walikuwa wanafanya pale?

Shahidi: Walikuwa wanajihusisha na vitendo vya umalaya.

Wakili: Ambavyo ni vipi?

Shahidi: Kuuza miili yao

Wakili: Wakati Wakili wa Serikali anakuongoza ulisema kuwa walimuuzia nani (miili)?

Shahidi: Sijasema

Wakili: Unajua walimuuzia nani?

Shahidi: Sijui

Wakili: Unajua walimuzia shilingi ngapi?

Shahidi: Sijui

Wakili: Unajua walikuwa wanauza sehemu gani ya miili yao?

Shahidi: Sijui

Wakili: Hiyo miili yao walikuwa wanauzia hapo barabarani?

Shahidi: Sijui

Wakili: Wakati wanauza hiyo miili wewe ulikuwa umekaa sehemu gani?

Shahidi: Sikumbuki

Wakili: Wao wakiuza miili wanabaki na nini?

Shahidi: Sijui

Wakili: Umemwambia mheshimiwa hakimu kwamba viashiria ni mavazi kwa kuwa mmojammoja walivaa nguo gani?

Shahidi: Sikumbuki.

Wakili: Umesema walikuwa wanauza miili, wanunuzi wako wapi?

Shahidi: Wapita njia

Wakili: Nakuuliza, wanunuzi wako wapi hapa?

Shahidi: Sijui

Wakili: Hao wanunuzi mliwakamata au hamkuwakamata?

Shahidi: Sijui, sikumbuki

Wakili: Kwa hiyo ni sahihi tukihitimisha kuwa wauzaji walikamatwa na wanunuzi hawakukamatwa?

Shahidi: Hawakukamatwa.

Wakili: Ni sahihi kwamba hamkuwakamata kwa sababu kununua sio kosa?

Shahidi: Hapana

Wakili Maria Mushi: Ulisema mliwakamata hawa washtakiwa kwa sababu walikuwa hawajavaa nguo za heshima, kuna sheria gani ambayo inazungumzia kuwa nguo za heshima ni zipi?

Shahidi: Siijui

Wakili: Kwa hiyo heshima kwa mtu mmoja sio lazima iwe heshima kwa mtu mwingine?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Kwa hiyo wewe uliona si nguo za heshima lakini inawezekana mimi ningeweza kuona ni nguo za heshima?

Shahidi: Inawezekana

Wakili: Unawafahamu Wamasai?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Unajua utamaduni wa mavazi yao?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Unajua mavazi yao wengine huwa wanaacha mapaja wazi?

Shahidi: Ndiyo

Wakili: Kwa hiyo hayo mavazi yao ni heshima au si heshima?

Shahidi: Sijawahi kuwaona.

Kesi hiyo itaendelea kesho Ijumaa Juni 28, 2024