Kikwete atimiza miaka 72, aanza siku kwa mazoezi
Muktasari:
- Kikwete atimiza miaka 72 leo, aanza siku kwa mazoezi ya kukimbia nyumbani kwake Msoga mkoani Pwani.
Dar es Salaam. Rais mstaafu wa Awamu ya nne Jakaya Kikwete ambaye leo anaadhimisha miaka 72 ya kuzaliwa kwake ameanza siku hiyo kwa kufanya mazoezi ya kutembea kilomita tano.
Kikwete ambaye anaadhimisha siku yake ya kuzaliwa akiwa nyumbani kwake Msoga mkoani Pwani, ameonyesha furaha yake kutimiza umri huo akiwa na afya njema.
“Haya ndiyo maisha yangu ya kila siku asubuhi, tukiamka tunazunguka kuna vilima vikali hapa tunapanda na kushuka,”amesema Kikwete
Akiwa anatembea njiani tukio ambalo limerushwa moja kwa moja na Clouds Media Group, Kikwete ameonekana akizungumza na watu aliokuwa akipishana nao njiani.
Rais huyo mstaafu ameonyesha pia maeneo mbalimbali katika kijiji hicho ambayo yana historia katika maisha yake ikiwemo nyumba aliyozaliwa, shule ya msingi aliyosoma na sehemu alizocheza.