Kitabu cha historia ya Komba kuzinduliwa
Aliyekuwa Mbunge wa Mbinga Magharibi, marehemu Kapteni John Komba
Muktasari:
Akizungumzia suala hilo, mjane wa Komba, Salome Komba (60) amesema leo jijini Dar es Salaam kuwa uzinduzi wa kitabu hicho unatarajiwa kufanyika Februari 28, mwaka huu, tukio litakaloendana na kumbukumbu ya kifo cha kada huyo wa Chama cha Mapinduzi (CCM).
Kitabu kinachoelezea historia ya maisha ya aliyekuwa Mbunge wa Mbinga Magharibi, marehemu Kapteni John Komba kinatarajiwa kuzinduliwa mwishoni mwa mwezi huu, familia yake yaeleza leo.
Akizungumzia suala hilo, mjane wa Komba, Salome Komba (60) amesema leo jijini Dar es Salaam kuwa uzinduzi wa kitabu hicho unatarajiwa kufanyika Februari 28, mwaka huu, tukio litakaloendana na kumbukumbu ya kifo cha kada huyo wa Chama cha Mapinduzi (CCM).
Akitoa picha ya namna kitabu kitakavyokuwa, Salome Komba amesema kitakuwa na kurasa 80 na kimeandikwa na Yusuf Halimoja ambaye ameelezea kwa kina historia ya Komba kuanzia kuzaliwa kwake, maisha yake na hadi kifo chake.
“Na sisi kama familia tuliamua ni vyema kuendeleza pale alipoishia na hivyo katika kumbukumbu ya Februari, mwaka huu tutakizindua kitabu hicho,” amesema.
Amesema marehemu mumewe alikuwa mbunge wa Mbinga Magharibi kwa kipindi cha miaka 10; kuanzia 2005 hadi 2015 na alikuwa mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM kwa miaka 28.
“Kitabu hiki marehemu Komba alianza kukiandika tangu mwaka 2002 na alitaka kukizindua mwaka 2014 lakini kutokana na sababu zilizo nje ya uwezo wake aliahirisha kukizindua,” Salome ameongeza.