Kodi zawadi michezo ya kubahatisha kupunguzwa, ya ubashiri wa matokeo kuongezwa

Kodi zawadi michezo ya kubahatisha kupunguzwa, ya ubashiri wa matokeo kuongezwa

Muktasari:

  • Serikali amependekeza kupunguzwa kwa kiwango cha kodi katika michezo ya kubahatisha kwenye zawadi ya ushindi  kutoka asilimia 20 hadi asilimia 15.

Dar es Salaam.  Serikali amependekeza kupunguzwa kwa kiwango cha kodi katika michezo ya kubahatisha kwenye zawadi ya ushindi  kutoka asilimia 20 hadi asilimia 15.

Pia,  imependekeza ongezeko la kiwango cha kodi katika michezo ya kubahatisha ya ubashiri wa matokeo ya michezo kwa mapato ghafi kutoka asilimia 25 ya mauzo ghafi hadi asilimia 30.

Hayo yamesemwa leo Alhamisi Juni 10, 2020 na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba alipokuwa akiwasilisha bungeni bajeti kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2021/22.

“Ongeza la kiwango cha kodi katika michezo ya kubahatisha ya ubashiri wa matokeo ya michezo kwa mapato ghafi kutoka asilimia 25 ya mauzo ghafi hadi asilimia 30,” amesema Nchemba.

Amesema ongezeko la asilimia tano litakwenda kwenye mfuko wa maendeleo ya michezo kwa ajili ya kuendeleza michezo nchini. 

Pia, kutozwa kwa kodi katika michezo ya kubahatisha kwa asilimia 10 ya mapato ghafi kwenye michezo ya kubahatisha inayoendeshwa kwa kompyuta.

Vilevile, kutozwa kodi kwa michezo ya kubahatisha kwa asilimia 10 ya mapato ghafi kwenye michezo ya kubahatisha iliyo chini ya majaribio. 

Lengo la hatua hiyo  ni kuleta usawa wa utozaji kodi katika michezo ya kubahatisha.

“Hatua hizi za marekebisho ya michezo ya kubahatisha zinatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha shilingi milioni 14,925.38,” amesema Nchemba.

Imeandikwa na Mariam Mbwana, Mwananchi