Leipzig kutazamwa na mashabiki 999

Muktasari:

Mamlaka jijini Leipzig zimetoa ruhusa ya kuingiza mashabiki wachache kulinganisha na wanaoruhusiwa kuona mechi za nyumbani za Bundesliga kutokana na maambukizi ya virusi vya corona kuongezeka.

 

Berlin, Ujerumani. RB Leipzig itaruhusiwa kuingiza mashabiki 999 katika uwanja wa Red Bull Arena wakati itakapocheza mechi yake ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa wa soka Ulaya dhidi ya Basaksehir ya Instanbul leo.

Licha ya kuongezek akwa idadi ya maambukizi ya virusi vya corona nchini Ujerumani, mamlaka jijini Leipzig zimetoa ruhusa kwa kuingiza hadi mashabiki 999, ikiwa ni idadi ndogo kulingana na ya kawaida ya mashabiki 8,500 wanaoruhusiwa kuangalia mechi za nyumbani za Ligi Kuu ya Ujerumani, Bundesliga.

Wastani wa siku saba wa maambukizi ya virusi hivyo jijini Leipzig hadi kufikia jana ilikuwa inakaribia watu 20 kati ya 100,000, ikiwa ni ndogo zaidi kulinganisha na Berlin ambako ni watu 87 na Munich ambako maambukizi ni watu 70.

Mabingwa watetezi wa Ulaya, Bayern Munich watakutana na Atletico Madrid Jumatano lakini mashabiki hawataruhusiwa kuingia uwanja wa Allianz Arena kuona mechi hiyo.

Leipzig, ambao wanaongoza Bundesliga, wamepania kupata ushindi kabla ya kwenda kuvaana na Manchester United, ambayo msimu uliopita iliishia nusu fainali, na baadaye kuwa mwenyeji wa Paris Saint Germain -- ambayo iliwafunga katika nusu fainali ya msimu uliopita.

"Tunajua tuko katika kundi lenye changamoto," alisema kocha wa Leipzig, Julian Nagelsmann.

Leipzig ilifika nusu fainali mapema mwaka huu baada ya kuzishinda Tottenham na Atletico Madrid, ikiwaimefika hatua hiyo kwa mara ya kwanza.

"Ni kitu cha ajabu kwanza (hali ya kukutana na vigogo) inaanza tena wakati huu, lakini tunasubiri kupambana nayo," alisema Nagelsmann, ikiwa ni siku 63 tu baada ya kufungwa na PSG.

Leipzig ilijiandaa kwa mchezo huo kwa ushindi mzuri wa mabai 2-0 dhidi ya Augsburg Jumamosi na kuendelea kukalia kilele cha Bundesliga, huku beki wa kushoto anayechezea klabu hiyo kwa mkopo kutoka Manchester City, Angelino na mshambuliaji wa Denmark, Yussuf Poulsen wafunga mabao.