Mafuriko yaua watatu, 300 wakosa makazi Kyela

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera akizungumza na wananchi waliokumbwa na mafuriko na makazi yao kusombwa na maji katika kijiji cha Kabanga kata ya Katumba Songwe ,Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya .Picha na Hawa Mathias.

Muktasari:

Watu watatu wamefariki dunia na wengine 300 wamekosa makazi baada ya nyumba zao kusombwa na maji kutokana na mvua kubwa zilizonyesha na kusababisha mafuriko katika kijiji cha Kabanga kata ya Katumba Songwe, Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya.

Kyela. Watu watatu wamefariki dunia na wengine 300 wamekosa makazi baada ya nyumba zao kusombwa na maji kutokana na mvua kubwa zilizonyesha na kusababisha mafuriko katika kijiji cha Kabanga kata ya Katumba Songwe, Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya.

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera amethibitisha kutokea vifo hivyo akisema mvua hiyo iliyonyesha Aprili 27 na 28 ilisababisha mafuriko.

Homera amesema hayo leo Jumamosi Aprili 30, 2022 baada ya kutembelea kituo cha pamoja cha forodha kati ya Tanzania na Malawi na kuona hali ya athari za mafuriko katika kata ya Katumba Songwe.

“Serikali imepokea kwa masikitiko makubwa tukio la kaya zaidi ya 249 makazi yao yamebomoka kutokana na mvuazilizonyesha kwa muda wa siku mbili mafululizo'' amesema.

Amesema kuwa kama mkoa unaendelea kujipanga kuona namna na kuwasaidia watu ambao wamekosa makazi, na kwamba wanawasiliana na ofisi ya Waziri Mkuu kutengo cha Maafa ili kupata maelekezo.

''Kama mkoa tunayo mahitaji kama maeneo ya kujisitiri watu ambao makazi yao yamebomolewa na mafuriko kwa sasa tayari wilaya inaendelea na utaratibu wa kuhakikisha chakula kinapatikana na mahitaji mengine ''amesema.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kyela, Ezekiel Magehema amesema kuwa mafuriko hayo yameathiri zaidi ya hekta 10,616 za zao la mpunga na mahindi ambazo zimesombwa na maji pamoja na mifugo.

Magehema amesema kuwa kutokana na changamoto hiyo tayari kamati ya maafa imetenga maeneo ambayo wamewekwa waliokosa makazi ikiwa ni pamoja na kuwapa mahitaji ya chakula na malazi.