Mahakama yataka upelelezi kesi ya Mwakabibi na mwenzake uharakishwe
Muktasari:
- Kwa mara ya kwanza, Mwakabibi na Haule walifikishwa mahakamani hapo Agosti 20, 2021 wakikabiliwa na mashtaka mawili ya matumizi mabaya ya madaraka wakiwa watumishi wa Serikali.
Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imeutaka upande wa mashtaka kuharakisha upelelezi katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke, Lusubilo Mwakabibi na Mratibu wa Mradi wa Uendelezaji Jiji la Dar es Salaam (DMDP), Edward Haule.
Mwakabibi na Haule, wanakabiliwa na mashtaka mawili ya matumizi mabaya ya madaraka wakiwa watumishi wa Serikali, katika kesi ya Uhujumu Uchumi namba 73/2021.
Amri hiyo imetolewa leo, Oktoba 19, 2023 na Hakimu Mkazi Mkuu, Evodia Kyaruzi, baada ya Serikali kudai kuwa upelelezi wa shauri hilo, upo katika hatua za mwisho kukamilika.
“Upande wa mashtaka mjitahidi kukamilisha kwa wakati kesi hii, maana maahirisho yamekuwa too much (yamezidi),” amesema Hakimu Kyaruzi.
Awali, wakili wa Serikali, Winiwa Samsoni akishirikiana na Monica Ndekidemi alidai kuwa shauri hilo limeitwa kwa ajili ya kutajwa na upelelezi wake upo katika hatua za mwisho.
“Kesi hii imekuja kwa ajili ya kutajwa, upelelezi wake bado haujakamilika, lakini tumeambia upelelezi upo katika hatua za mwisho kukamilika na mara ya mwisho, jalada hii lilikuwa ofisi ya DPP kwa ajili ya kufanyiwa kazi, hiyo tunaomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa” amedai Samson.
Hakimu Kyaruzi baada ya kusikiliza maelezo hayo, ameahirisha kesi hadi Novemba 21, 2023 itakapotajwa na washtakiwa wote wapo nje kwa dhamana.
Katika kesi ya msingi, shtaka la kwanza ambalo ni matumizi mabaya ya ofisi, washtakiwa wanaodaiwa kutenda kosa hilo, kati ya Machi 2020 na Machi 2021 katika Manispaa ya Temeke.
Siku hiyo, Mwakabibi akiwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke na Haule akiwa Mratibu wa Mradi wa DMDP na wakiwa waajiriwa wa manispaa hiyo katika utekelezaji wa ardhi walielekeza ujenzi wa stendi ya mabasi eneo la Buza, kiwanja ambacho kinamilikiwa na Dayosisi ya Kanisa la Anglikana bila kuwa na ruhusa.
Shtaka la pili ni matumizi mabaya ya madaraka, tukio wanaodaiwa kulitenda Machi 2020 na Machi 2021 katika eneo hilo, ambapo washtakiwa kwa makusudi walitumia madaraka yao vibaya kinyume na kifungu cha 3(1) cha Sheria ya Ardhi na kifungu cha 3,4,5,7 na 11 cha Sheria ya Ardhi ya mwaka 2019, ambapo waliruhusu ujenzi wa kituo kufanyika katika eneo linalomilikiwa na kanisa.
Kwa mara ya kwanza, washtakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo Agosti 20, 2021 na kusomewa mashtaka yanayowakabili.