Majeruhi ajali ya ndege ziwa Victoria asimulia ajali ilivyotokea

Mmoja wa abiria walionusurika katika ajali ya ndege ya Precision Air, Richard Komba

Muktasari:

  • Ndege hiyo ya Precision Air iliyokuwa inatoka Dar es Salaam kwenda Bukoba imepata ajali katika ziwa Victoria leo Jumapili Novemba 6, 2022 ilipokuwa ikijaribu kutua na kusababisha vifo vya watu 19.

Dar es Salaam. Mmoja wa abiria walionusurika katika ajali ya ndege ya Precision Air ambayo imepata ajali katika ziwa Victoria na kusababisha vifo vya watu 19, amesimulia kilichotokea kabla ya ndege hiyo kuanguka.

 Akizungumza na waandishi wa habari katika hospitali ya rufaa ya Kagera leo Novemba 6, Richard Komba amesema kuwa hali ya hewa kutoka Mwanza mpaka Bukoba ilikuwa mbaya tofauti na tofauti na hali iliyokuwa kutoka Dar es Salaam hadi Mwananza.

Akiwa kwenye kitanda hospitalini, Komba anasema waliondoka Dar es Salaam karibu 12: 15 asubuhi hali ya hewa ikiwa nzuri.

"Toka Dar es Salaam mpaka Mwanza hali ya hewa ilikuwa nzuri, lakini wakati tumetoka Mwanza kuja Bukoba hali haikuwa nzuri, kwa hiyo wakati tunakaribia kushuka ikaonekana hatuwezi kushuka” amesema nakuongeza

“Rubani akalazimika kuzunguka, tumeenda mpaka maeneo ya Misenyi akatupa taarifa kwamba hali ya hewa sio nzuri, mvua inanyesha kwa hiyo akasema anajaribu kurudi tena kama hali bado itakuwa hivyo itabidi apelike ndege Mwanza” amesema.

Komba amesema baada ya ndege kutumbukia kwenye maji yalianza kuingia kwenye ndege ambapo yalianza kuwaathiri waliokaa mbele.

Amesema yeye alikuwa amekaa nyuma ambapo mhudumu alifungua mlango ndipo wakaanza kutoka.

New Content Item (1)
New Content Item (1)

Kufuatia ajali hiyo, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametangaza vifo vya watu 19, huku wengine 26 wakiwa wamenusurika.

Hata hivyo, Majaliwa akiwa katika eneo la ajali ya ndege ya Precision Air ameagiza kufanyika uchunguzi wa idadi kamili ya watu waliokuwa kwenye ndege hiyo.

Majaliwa ametoa agizo hilo baada ya kuwepo kwa taarifa tofauti ambapo ametangaza idadi ya vifo 19 huku 26 wakinusurika ambapo inafanya jumla ya watu wanaohusishwa kwenye ajali hiyo kuwa 45.

Awali taarifa rasmi kutoka Shirika la Precision Air na Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Albert Chalamila zilisema kuwa watu waliokuwa kwenye ndege hiyo walikuwa 43, kati yao abiria 39, wahudumu wawili na marubani wawili.

Ndege hiyo iliyopata ajali ya kutumbukia Ziwa Victoria, mita 100 kabla ya kutua Uwanja wa Ndege wa Bukoba, Mkoa wa Kagera.