Watu 19 wafariki ajali ya ndege Ziwa Victoria

Muktasari:

  • Ndege hiyo ya Precision Air ambayo ilikuwa na watu 43 ilikuwa ikitoka Dar es Salaam kwenda Bukoba.

Bukoba. Watu 19 wakiwemo abiria na wahudumu wamefariki dunia katika ajali ya ndege ya shirika la Ndege la Precision Air iliyotokea asubuhi ya leo Jumapili Novemba 6, 2022.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametangaza vifo hivyo leo jioni baada ya kuwasili kwenye eneo ilipotokea ajali hiyo.

Ajali hiyo imetokea leo asubuhi kutokana na ndege hiyo kushindwa kutua katika uwanja wa ndege wa Bukoba, Mkoa wa Kagera na kutumbukia Ziwa Victoria ambalo lipo karibu na uwanja huo.

Ndege hiyo ilikuwa na watu 43, kati yao 39 wakiwa abiria, marubani wawili na wahudumu wawili ambapo tayari 28 wameokolewa.

Awali Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Issessanda Kaniki alithibitisha kutokea kwa vifo vya watu watatu kabla ya Majaliwa kufika na kutangaza idadi ya waliokufa kuwa ni 19.

Ndege hiyo ya Precision Air ambayo ilikuwa na watu 43 ilikuwa ikitoka Dar es Salaam kwenda Bukoba.


Endelea kufuatilia mitandao yetu kwa habari zaidi