Mbunge apigia chapuo zao la Kahawa Hai
Mbunge wa Hai, Saashisha Mafuwe
Muktasari:
- Mbunge wa Hai, Saashisha Mafuwe amewataka wananchi wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro kuhakikisha wanalima zao la kahawa huku akijivunia zao hilo kufanya vizuri Kimataifa.
Hai. Mbunge wa Hai, Saashisha Mafuwe amewataka wananchi wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro kuhakikisha wanalima zao la kahawa huku akijivunia zao hilo kufanya vizuri Kimataifa.
Mafuwe ametoa rai hiyo leo Jumanne Machi 8,2022 akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Nnronga kilichopo Kata ya Machame Magharibi wilayani humo.
"Wazee wangu naomba mpande kahawa maana tutaanza kukagua kwa nguvu mbegu za kahawa tumegawa na bado nimepata miche mingine. Nimemwomba Waziri amenipa miche 343,000 tulikuwa tunasubiri tuu mvua ziishe watupe hiyo miche.
"Juzi mmesikia kahawa nzuri imetangazwa duniani imetoka hapa kwetu Lyamungo, bei ya kahawa inazidi kupanda kila siku. Nimeshapelekea mapendekezo yangu kuhusu kahawa, naomba pandeni kahawa .
"Hili zao la kahawa ndio limetupa heshima Mkoa huu wa Kilimanjaro ndio maana mnaona napambana na vyama vya ushirika,tumeshavunja mikataba ya ovyo kwenye jimbo hili la Hai na sasa hivi kimebaki tuu chama kimoja " amesema Mafuwe
Mmoja wa wananchi wa kijiji hicho, James Lema amesema wamekuwa wakilima zao hilo bila faida hali ambayo imekuwa ikiwakatisha tamaa ya kulima kutokana na kuporomoka kwa bei ya kahawa.