Mbunge CCM ataka muda wa kuthibitisha wagonjwa wa akili kupunguza
Muktasari:
Mbunge wa viti maalumu CCM, Lucy Mayenga ameitaka Serikali kupunguza muda wa kuthibitisha wagonjwa wa akili walioko kwenye magereza mbalimbali nchini.
Dodoma. Mbunge wa viti maalumu CCM, Lucy Mayenga ameitaka Serikali kupunguza muda wa kuthibitisha wagonjwa wa akili walioko kwenye magereza mbalimbali nchini.
Mayenga ameyasema hayo leo Jumatano Februari 3, 2021 wakati akiuliza swali la nyongeza bungeni mjini Dodoma katika kikao cha pili cha Bunge la 12.
Amesema kuna wafungwa wanaougua ugonjwa wa akili na wapo katika kundi la kisheria lakini udhibitisho umekuwa ukichukua muda mrefu huku akihoji mkakati wa Serikali kupunguza muda wa kuwahudumia wagonjwa hao.
Akijibu swali hilo Waziri wa Afya, Dk Dorothy Gwajima amesema wamelichukua na watalifanyia kazi ili watu hao waweze kupata huduma mapema.
Katika swali la msingi, mbunge wa viti maalum CCM, Mariam Kisangi amesema Tanzania imekuwa na ongezeko kubwa la wagonjwa wa afya ya akili, “nini chanzo cha ugonjwa huo, je Serikali ina utaratibu gani wa kuwasaidia wagonjwa wa afya ya akili.”
Akijibu swali hilo naibu Waziri wa Afya, Dk Godwin Mollel amesema kitaalamu hakuna sababu moja inayoweza kusababisha ugonjwa wa afya ya akili.
Amesema sababu za kibailojia, uwepo wa vinasaba katika mwili vinaongeza uwezekano wa mtu kupata ugonjwa wa afya ya akili.
Nyingine ni maradhi ya muda mrefu na matumizi ya vilevi kama bangi, pombe na aina nyingine za vilevi zinaweza kuwa vichocheo hasa kwa mtu mwenye vinasaba vya uhatarishi wa ugonjwa.
Dk Mollel amesema Serikali iliandaa sheria inayosimamia utoaji wa huduma za afya ya akili mwaka 2008 inayotoa mwongozo na utaratibu wa namna ya kuwapokea na kuwahudumia watu wenye ugonjwa wa akili.
Pia Serikali imehakikisha kuwa huduma za matibabu ya ugonjwa wa afya ya akili ikiwa ni pamoja na dawa zinatolewa kuanzia ngazi ya hospitali za rufaa za mikoa hadi hospitali maalum ya Taifa ya afya ya akili Mirembe.
Amesema pia Serikali itaendelea kutoa elimu kuhusu ushiriki wa wazazi katika kuwalea watoto na kuongeza udahili wa wanafunzi wa uzamivu kutoka wanafunzi watatu hadi watano ilipofika mwaka 2015 na kufikia udahili wa wanafunzi 10 hadi 15 kwa mwaka ilipofika 2020.
Amesema pia Serikali imeongeza idadi ya vyuo vikuu vinavyotoa shahada ya uzamivu kutoka kimoja mwaka 2015 hadi kufikia vyuo vitatu mwaka 2020.