Mjamzito anyongwa hadi kufa, wawili wauawa Geita

Kamanda wa polisi Mkoa wa Geita, Mponjoli Mwabulambo

Muktasari:

Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita nchini Tanzania linaendelea na uchunguzi wa matukio matatu ya vifo vilivyotokea katika mazingira tofauti likiwamo la mama mjamzito kuuawa kwa kunyongwa na watu wasiojulikana.

Geita. Watu watatu nchini Tanzania wameuawa kwa matukio matatu tofauti likiwamo la mama mwenye ujauzito unaokadiriwa kuwa na miezi 8-9 kuuawa kwa kunyongwa na watu wasio julikana

Taarifa iliyotolewa leo Ijumaa Machi 20,2020 na kamanda wa polisi Mkoa wa Geita, Mponjoli Mwabulambo amesema mwanamke huyo Rebeka James (28) mkazi wa kijiji cha Masumbwe alivunjwa shingo kwa kunyongwa na watu wasio julikana.

Kamanda huyo amesema chanzo cha mauaji hayo kinasadikiwa kuwa ni wivu wa mapenzi na kwamba waliotekeleza tukio hilo walivunja mlango wa chumba anachoishi mwenyewe.

Tukio jingine ni watu wasio julikana kumuua kwa kumpiga mapanga Charles Kahindi (34) mkazi wa mtaa wa Katoro kata ya Katoro wilayani Geita.

Tukio hilo limetokea jana Alhamisi Machi 19,2020  nyumbani kwa mfanyabiashara huyo ambapo marehemu akiwa na mkewe wamelala chumbani alivamiwa na watu wasiojulikana na kumkata kata mapanga kichwani shingoni na mkono wa kushoto.

Tukio jingine ni mwanaume anayekadiriwa kuwa na umri  kati ya miaka 25-30 kuuawa kwa kupingwa na wananchi waliojichukulia sheria mkononi baada ya kudaiwa kuiba solar, runinga na flash.