Mtakuwa yapunguza ukatili wa kijinsia Rombo
Muktasari:
Wadau wa haki za binadamu, wananchi Wilaya ya Rombo Mkoani Kilimanjaro wamesema kuanzishwa kwa mpango wa Taifa wa kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto (Mtakuwa) umepunguza kwa kiasi kikubwa ukatili wa kijinsia wilayani humo.
Rombo. Wadau wa haki za binadamu, wananchi Wilaya ya Rombo Mkoani Kilimanjaro wamesema kuanzishwa kwa mpango wa Taifa wa kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto (Mtakuwa) umepunguza kwa kiasi kikubwa ukatili wa kijinsia wilayani humo.
Wakizungumza na Mwananchi kwa nyakati tofauti wadau hao wa haki za binadamu wamesema matukio mengi ya ukatili yaliyokuwa yakifanywa Wilayani Rombo yanatokana na wananchi kutokuwa na elimu na kuamua kujichukulia sheria mkononi.
Mwenyekiti wa wasaidizi wa kisheria Wilaya ya Rombo, Remmy Shirima ,amesema Kamati ya Mtakuwa iliyoanzishwa kwa ajili ya kutokomeza ukatili dhidi ya wanawke na watoto imesaidia sana kupunguza matukio ya ukatili kwenye jamii.
"Kamati hii imepunguza ukatili kwenye jamii kutokana na kuwa na wajumbe wengi kuanzia ngazi za kata hadi Mkoa kwahiyo jamii sasa jamii imeelimika na bado elimu inaendelea kutolewa katika maeneo mbalimbali ," amesema Shirima
Mkurugenzi wa shirika la kisheria na kutetea haki za binadamu (Ajiso)Mkoa wa Kilimanjaro ,Virginia Silayo amesema mpango huo wa MTAKUWA umepunguza ukatili wa kijinsia kutokana na elimu ya ushirikishwaji kwa wadau wa ngazi mbalimbali za jamii.
"Nashauri Mtakuwa awamu ya pili itakayoanza mwakani na mashirika yasiyo ya kiserikali kutoa mafunzo kwenye kamati za Mtakuwa ianzie ngazi za vijiji kwasababu awamu ya kwanza tumefanya zaidi kwenye mikoa na Halmashauri na kidogo kwenye Kata,"alisema Silayo
Mmoja wa wananchi wa kijiji cha Lesorroma,Adolfina Atanasi amesema mwanzoni kabla hawajapata elimu hiyo walikuwa wanaogopa kutoa ushirikiano pale tukio la ukatili linapojitokeza kwenye jamii kutokana na hofu.
"Sasa hivi baada ya kupata hii elimu ya Mtakuwa tumekuwa wajasiri kwasababu tumeelewa mambo mengi juu ya ukatili wa kijinsia na hii inatupa fursa ya kutoa ushirikiano pale ambapo panapotokea ukatili tunaripoti kwa haraka kwa wahusika,"alisema Adolfina
Mpango huo ambao ulianzishwa mwaka 2018 ulilenga kupunguza ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto kwa asilimia 50 ifikapo mwaka 2022.