Mtwara wapigwa msasa ulinzi wa watoto, wanawake
Wajumbe wa kamati za Ulinzi na Usalama wa Mtoto na Mwanamke ngazi ya Kata Katika Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara-Mikindani wa Kata za Mitengo, Magengeni, Jangwani na Kisungule wakiwa kwenye mafunzo. Picha na Florence Sanawa
Muktasari:
- Wajumbe 112 wa kamati za ulinzi na usalama wa mtoto na mwanamke ngazi ya Kata Katika Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara-Mikindani wamepatiwa mafunzo elekezi ili kuweza kutambua viashiria hatarishi vya ukatili.
Mtwara. Wajumbe 112 wa kamati za ulinzi na usalama wa mtoto na mwanamke ngazi ya kata katika Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara-Mikindani wamepatiwa mafunzo elekezi ya kupinga ukatili dhidi ya watoto na wanawake ili waweze kubaini viashiria hatarishi vya ukatili na kuviwasilisha sehemu husika.
Mafunzo hayo yamehusisha kata nane ambazo ni Kata ya Mitengo, Magengeni, Kisungule, Jangwani, Ufukoni, Naliendele, Majengo na Likombe ikiwa ni awamu ya pili ambapo mafunzo ya awali yalifanyika katika kata kumi zilizopo Manispaa ya Mtwara-Mkindani.
Akizungumza katika mafunzo ya siku tatu, Afisa Ustawi wa Jamii wa Manispaa ya Mtwara-Mikindani, Fatu Mapua amesema kamati hizo zinapaswa kutumia elimu waliyoipata katika kuelimisha jamii kuhusu kupinga ukatili dhidi ya Mtoto na Mwanamke na kuwasisistiza kufanya kazi kwa uzalendo.
Mapua amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo na uelewa wa kubaini na kuchukua hatua pale inapotokea kesi inayohusu ukatili.
Aidha, Mapua amezitaka kamati hizo kufanya kazi kwa kushirikiana na Kamati za mitaa, waalimu wa malezi, vikundi vya malezi vilivyopo mitaani ambavyo vitasaidia kutambua ishara mbalimbali za ukatili na kufuatilia maendeleo ya waathirika ili kulinda kizazi kipya dhidi ya ukatili
Kaimu Afisa Mtendaji Kata ya Ufukoni, Iddi Songea amesema kuwa mafunzo hayo yanaenda kubadilisha jamii kwakuwa sasa watu watajua nini wanapaswa wafanye hasa wanapoona viashiria vya ukatili ndani ya jamii.