Muliro: Ombeni lifti kwenye difenda za polisi

Muktasari:

  • Kauli ya Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro kuwataka wananchi kuacha kuogopa kuomba lifti kwenye difenda za polisi imeibua maoni tofauti ya wananchi huku wengine wakisema huo ni mtego.

Dar es Salaam. Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro amewataka wananchi kuacha woga wa kuomba lifti kwenye difenda za polisi kwa kile alichokieleza kuwa gari hizo ni mali ya umma.

Ameyasema hayo leoFebruari 14, 2023 wakati wa mahojiano katika kipindi cha Clouds360 kinacholushwa na televisheni ya Clouds.

“Kuna mtu alishawahi kuomba lift kwenye Difenda hakupewa? Kwanini wanapanda watuhumiwa tu. Kwanini raia wa kawaida hawaombi lift? Au walishawahi kulisimamisha wakanyimwa lift? kwa mfano Difenda linakwenda Bunju, Tegeta, Kunduchu, Kitunda au Mwanagati, Kivule analiona kabisa limeandikwa Polisi na wewe unakwenda maeneo hayo kwanini usilisimamishe ukaomba lift?,

Hayo magari ya umma kwani polisi ni nini? Si ni Taasisi ya Umma? Jaribu siku kulisimamisha kama utanyimwa lift",” alisema Muliro.

Kauli yake iliibua hisia tofauti kutoka kwa wafuatiliaji wa kipindi hicho ambapo kupitia mitandao ya kijamii walitoa mitazamo yao huku wengine wakienda mbali zaidi na kumtaka atoe namba za simu ili ikitokea vinginevyo wampigie simu.

@Dacotadelavida kupitia ukurasa wake aliandika “Mkuu nipe no (namba) yako kabisa nataka nijaribu wiki hiii.... na je umeshasema nao vijana wako.... maaana hawaeleweki mpaka jambo lije kukufikia wewe mkuu huku mtu yupo ndembe ndembe kama tambi kwa kipondo.

Ochamshama aliandika “Tatizo ukipanda watu watajua we mwizi.

@Official_pz aliandika “Unaweza omba lifti gari inakwenda Mbagala ghafla wanapigiwa simu kuna tukio Mwenge unashangaa gari imekoneshwa shwaa… safari ya Mwenge kuruka huwezi… unazurura wewe siku mzima mpaka utajuta kuomba lifti magari ya polisi.

@Afya_consultants alisema “Shida ni jirani zangu wakiniona basi watapiga simu nyumbani nimekamatwa.

@shirimaujenziboratz aliandika “Mbona kama mtego huu Dk (Daktari) aliniambia niwe natembea mkuu ili mwili wangu upungue.

@fredibenya9 aliandika @Polisi wako kama namba 6 ukiangalia kwa juu inasomeka tisa ukiangalia kwa chini inasomeka 6 hata iwe umbali kiasi gani mguu kwa mguu,” aliandika.

@happy_hour_delicacies alihoji “Inakushusha unapotaka au ikiwa speed inakulepeka inapoenda.

Wakati wengine wakionyesha hofu ya kutumia usafiri huo, @rajabuabdurrahman aliandika “Kamanda tumekuelewa sana tutaanza hilo jambo, ila waambie madereva wa difenda wakiwaona watoto wa shule waanze na hao kuwapa lifti mpaka shuleni.