Muswada wa bima ya afya kwa wote wasomwa bungeni

Muktasari:

  • Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote umewasilishwa bungeni ambapo mwajiri wa sekta ya umma na binafsi rasmi atapaswa kumsajili mwajiriwa katika skimu ya bima ya afya ndani ya siku 30 tangu kuanza kwa mkataba wa ajira.


Dodoma. Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote umewasilishwa bungeni ambapo mwajiri wa sekta ya umma na binafsi rasmi atapaswa kumsajili mwajiriwa katika skimu ya bima ya afya ndani ya siku 30 tangu kuanza kwa mkataba wa ajira.

Muswada huo uliosomwa kwa mara ya kwanza leo, Ijumaa Septemba 23,2022, utakwenda kujadiliwa katika kamati kabla ya kumalizia mchakato mwingine wa utungaji wa sheria.

Pamoja na mambo mengine unatoa masharti ya mwajiri wa sekta ya umma na sekta binafsi kuwasilisha katika skimu asilimia sita ya mshahara wa mwajiriwa, ambapo ndani yake mwajiri atachangia nusu au zaidi ya kiwango hicho, na kiwango kilichosalia kitachangiwa na mwajiriwa.

Aidha, waziri kwa kushauriana na waziri mwenye dhamana ya masuala ya fedha, ataainisha viwango vya uchangiaji kwa ajili ya sekta isiyo rasmi, kama itakavyoainishwa katika kanuni, kwa kuzingatia tathmini ya uhai na uendelevu wa skimu za bima ya afya katika utoaji wa kitita cha mafao ya msingi.

Pia muswada huo unabainisha kuwa waziri, kwa kushirikiana na mamlaka zinazohusika, na kwa kupitia kanuni, ataweka utaratibu na namna ya utambuzi wa watu wasio na uwezo.

Amesema watu watakaotambuliwa kama watu wasio na uwezo watakuwa na haki ya kujumuishwa chini ya skimu ya bima ya afya kwa namna itakayoainishwa kwenye kanuni.

Aidha, Waziri mwenye dhamana ya masuala ya fedha, kwa kushauriana na Waziri, ataainisha vyanzo mahususi kwa ajili ya ugharamiaji wa huduma za bima ya afya kwa watu wasio na uwezo.

Pia amesema iwapo mwanachama anayechangia kupitia makato ya mshahara wake atafariki, wategemezi wake wataendelea kunufaika na huduma kwa kipindi kitakachoinishwa katika kanuni.

“Iwapo mwanachama anachangia kwa utaratibu wa michango kwa mwaka atafariki, wategemezi wake wataendelea kunufaika na huduma kwa kipindi kilichosalia cha mkataba wa uanachama,”amesema.