Neema kwa wakulima wa korosho Lindi na Mtwara
Muktasari:
- Wakulima wa korosho katika mikoa ya Lindi na Mtwara wapo mbioni kupata uhakika wa masoko ya bidhaa zao kutokana na jumuiya ya wazalishaji wa zao hilo (Taruchina) kuanza mchakato wa ujenzi wa maghala na viwanda.
Lindi. Wakulima wa korosho katika mikoa ya Lindi na Mtwara wapo mbioni kupata uhakika wa masoko ya bidhaa zao kutokana na jumuiya ya wazalishaji wa zao hilo (Taruchina) kuanza mchakato wa ujenzi wa maghala na viwanda.
Hayo yameelezwa na katibu wa jumuiya hiyo, Storitorius Kamutu kwenye hafla ya kukabidhiwa eneo la ekari 100 kwa ajili ya ujenzi huo katika mtaa wa Tandangongoro manispaa ya Lindi iliyofanyika jana Jumanne Julai 6, 2021.
Amesema ujenzi katika eneo hilo utasaidia kuongeza thamani ya korosho na kupunguza tatizo la ajira kwa wakazi wa Lindi na mikoa jirani.
“Mpango ni kuwa na kituo kimoja cha upatikanaji bidhaa inayotokana na korosho na ujenzi wa viwanda zaidi ya 150 ili kuongeza thamani na kuongeza ajira kwa wakulima kwa faida.., sisi wenyewe tuna lengo la kubangua korosho zote zinazozalishwa na wakulima,” amesema Kamutu.
Mwenyekiti wa mtaa wa Tandangongoro, Abdallah Makumba amesema ujio wa mpango huo wa viwanda na maghala utaongeza wigo wa uzalishaji wa korosho baada kupatikana soko la uhakika na kuongeza mapato ya halmashauri.