Neema kwa wakulima wa korosho Lindi na Mtwara

Neema kwa wakulima wa korosho Lindi na Mtwara

Muktasari:

  • Wakulima wa korosho katika mikoa ya Lindi na Mtwara wapo mbioni kupata uhakika wa masoko ya bidhaa zao kutokana na jumuiya ya wazalishaji  wa zao hilo (Taruchina) kuanza mchakato wa ujenzi wa maghala na  viwanda.

Lindi. Wakulima wa korosho katika mikoa ya Lindi na Mtwara wapo mbioni kupata uhakika wa masoko ya bidhaa zao kutokana na jumuiya ya wazalishaji  wa zao hilo (Taruchina) kuanza mchakato wa ujenzi wa maghala na  viwanda.

Hayo yameelezwa na katibu wa jumuiya hiyo, Storitorius Kamutu  kwenye hafla ya kukabidhiwa  eneo la ekari 100  kwa ajili ya ujenzi huo katika mtaa wa Tandangongoro manispaa ya Lindi iliyofanyika jana Jumanne Julai 6, 2021.

Amesema ujenzi katika eneo hilo utasaidia kuongeza thamani ya korosho na kupunguza tatizo la ajira kwa wakazi wa Lindi  na mikoa jirani.

“Mpango ni  kuwa na kituo kimoja cha upatikanaji bidhaa  inayotokana na korosho na ujenzi wa viwanda zaidi ya 150  ili kuongeza thamani   na kuongeza ajira kwa wakulima kwa  faida.., sisi wenyewe tuna lengo la kubangua korosho zote zinazozalishwa na wakulima,” amesema Kamutu.

Mwenyekiti wa mtaa wa  Tandangongoro, Abdallah Makumba  amesema ujio wa mpango huo wa viwanda na maghala  utaongeza wigo wa uzalishaji wa korosho baada kupatikana soko la uhakika na kuongeza mapato ya halmashauri.