PAC yaingilia kati deni la Tanesco kwa TPDC

Muktasari:

Tanesco inadaiwa deni hilo na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kutokana na mradi wa bomba dogo la gesi.

Dodoma. Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imeahidi kujadili deni linalodaiwa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) linalofikia Sh300.6 bilioni.

Tanesco inadaiwa deni hilo na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kutokana na mradi wa bomba dogo la gesi.

Mwenyekiti wa PAC, Naghenjwa Kaboyoka amesema wameipokea ripoti ya TPDC na kutokana na umuhimu wake, kamati hiyo itakaa kujadili na kutoa uamuzi.

“Kama unavyoona, shirika hili limepewa jukumu kubwa la kuhakikisha linasambaza gesi kwa Watanzania ili kuwezesha utunzaji wa mazingira. Ni lazima tuwasaidie waweze kupata fedha za maendeleo,” alisema.

Awali, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco, Dk Tito Mwinuka amesema deni hilo linaendelea kulipwa kidogokidogo na kwamba hata wiki iliyopita walipunguza.

Akizungumza katika mkutano wa TPDC na PAC, Mwenyekiti wa bodi wa shirika hilo, Profesa Sufian Bukurura amesema  pia wanaiomba kamati hiyo kuwasaidia ili wapate fedha za maendeleo ambazo Serikali iliahidi kuzitoa kama njia ya kukuza mtaji.

“Tungezipata hizo fedha tungeweza kulipa deni la Sh100 bilioni tunalodaiwa na taasisi mbalimbali,” amesema.