Rais Samia afurahishwa na Mbowe Baraza la Eid

Rais Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi mbalimbali pamoja na Waumini wa dini ya Kiislamu kwenye Baraza la Eid El-Fitr leo Junamosi Aprili 22, 2023 katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Muktasari:

  • Rais Samia ameeleza kufurahishwa kwake kwa viongozi wa vyama vya Chadema na CUF kujumuika katika Baraza la Eid jijini Dar es Salaam, akisema miaka iliyopita jambo hilo lisingewezekana.

Dar es Salaam. Rais Samia Suluhusu Hassan ameeleza kufurahishwa kwake kuwaona viongozi tofauti wa siasa, akiwemo Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe na Mwenyekiti wa CUF, Ibrahim Lipumba.

Samia ameyasema hayo leo Aprili 22 alipokuwa akihutubia Baraza la Eid lililoandaliwa na Baraza la Waislamu Tanzania (Bakwata) na kufanyika kitaifa jijini Dar es Salaam.

Kabla hajaanza hotuba yake, Rais Samia amewakaribisha Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba kusalimia baraza hilo.

Alipokuwa akihutubia baraza hilo, Rais Samia aliwataka Watanzania wote kuendeleza matendo mema waliyoishi wakati wa mfungo huo huku akiahidi kuunganisha taifa kwa umoja na mshikamano.

“Leo nawaona hapa wageni wengi, wanasiasa, mzee wa upako, kiongozi wa wahindu, hii ndio Tanzania tunayoitaka, naomba Mwenyezi Mungu aendelee kunilinda ili kuilinda Tanzania hii (yenye umoja),” amesema Rais Samia.

“Sisi viongozi wa kisiasa inatupatia amani na furaha, haikuwa rahisi mwaka jana na juzi kumuona Mbowe yupo hapa lakini leo tuko naye hapa kwa moyo msafi, amepanda jukwaani ameongea vizuri sana huko ndiko tunakotaka kuelekea kujifunza mafunzo tunayopata ndani ya dini zetu,”

Akitoa salamu katika baraza hilo, Mbowe amesisitiza kuendeleza matendo mema waliyoishi katika mwezi mtukufu ikiwamo kuimarisha umoja na ushirikiano.

Naye Profesa Lipumba akisisitiza uongozi bora wa rais Samia unahitaji kutiwa moyo. “Tuendelee kumtia moyo katika kazi yake anayofainya (rais), awe na ujasiri wa kufanya mapenzi mema kwa watanzania wote ikiwamo suala la Tume huru.”