Rais Samia akataa tabia ya kutukuzwa

Rais Samia Suluhu Hassan

Muktasari:

  • Rais Samia Suluhu Hassan amesema hana tabia ya kutukuzwa wala kulinganishwa na Mungu na kwamba atajitahidi kuwa na hekima na uvumilivu wa kusikiliza maoni ya wengine.

  


Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan amesema hana tabia ya kutukuzwa wala kulinganishwa na Mungu na kwamba atajitahidi kuwa na hekima na uvumilivu wa kusikiliza maoni ya wengine.

Rais Samia Amesema hayo leo Jumanne Februari 22, 2022 katika sherehe za Jubilee ya miaka yake 25 ya Askofu Severine Niwemugizi inayofanyika wilayani Ngara mkoani Kagera.

Alikuwa akijibu kauli iliyotolewa na Askofu wa Jimbo Katoliki la Rulenge-Ngara, Severine Niwemugizi aliyeemuomba Rais Samia kutokubali kulinganishwa na Mungu kwa namna yoyote ile.

“Baba Askofu katika kufunga hotuba yako umeniasa mambo ya kukataa kutukuzwa na mimi nataka nikuahidi mbele ya umma huu kwamba, hii si tabia yangu na ninajitahidi kujishusha niwe sawa na wengine. Maana utumishi huu kama mipango ya Mungu ilivyo ameniweka hapa niwatumikie na siyo nijitukuze kwenu kwahiyo nitawatumikia,” amesema Rais Samia.

Amesema atajitahidi kuwa na hekima na uvumilivu na awe na sikio la kusikiliza yale yanayosemwa na wengine.