Rais Samia atengua uteuzi wa Chalamila

Muktasari:

Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan leo Ijumaa Juni 11, 2021 amefanya mabadiliko madogo ya wakuu wa mikoa na kuteua baadhi ya viongozi wengine.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan leo Ijumaa Juni 11, 2021 amefanya mabadiliko madogo ya wakuu wa mikoa na kuteua baadhi ya viongozi wengine.

Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Jaffar Haniu inaeleza kuwa kiongozi mkuu huyo wa nchi amemhamisha mkuu wa Mkoa wa Mara, Robert Gabriel kuwa mkuu wa Mkoa wa Mwanza kuchukua nafasi ya Albert Chalamila ambaye uteuzi wake umetenguliwa.

“Gabriel anahamia Mwanza  kuchukua nafasi ya Chalamila ambaye uteuzi wake umetenguliwa,” inaeleza taarifa hiyo ikibainisha kuwa mkuu wa Mkoa wa Tabora, Ally Hapi amehamishiwa Mkoa wa Mara kuchukua nafasi ya Gabriel.

Taarifa hiyo inaeleza kuwa Rais Samia amemteua katibu tawala wa Mkoa wa Shinyanga, Batilda Buriani kuwa mkuu mpya wa Mkoa wa Tabora akichukua nafasi ya Hapi.

Katika taarifa hiyo, katibu tawala wa Wilaya ya Simanjiro, Zuwena Jiri ameteuliwa kuwa katibu tawala Mkoa wa Shinyanga kuchukua nafasi ya Buriani.

Taarifa hiyo inaeleza kuwa tarehe ya kuapishwa viongozi hao wapya itatangazwa baadaye.