RC Kagaigai awataka Kia kuharakisha uagizaji magari ya zimamoto
Muktasari:
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Stephen Kagaigai ameutaka uongozi wa uwanja wa ndege wa Kimataifa (KIA) kuharakisha uagizwaji wa magari mawili ya kisasa ya zimamoto ili uwanja huo uendelee kuwa na usalama zaidi.
Hai. Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Stephen Kagaigai ameutaka uongozi wa uwanja wa ndege wa Kimataifa (KIA) kuharakisha uagizwaji wa magari mawili ya kisasa ya zimamoto ili uwanja huo uendelee kuwa na usalama zaidi.
Kagaigai ameyasema hayo leo wakati alipotembelea uwanja huo wa ndege kujiona shughuli mbalimbali zinazoendelea ambapo Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa uwanja huo, Christina Mwakatobe alieleza kuwa magari yaliyopo baadhi yamekuwa ni chakavu na kutishia hadhi ya usalama wa uwanja huo.
"Nimefarijika sana kuona namna kampuni hii inavyohakisha kuna usalama wa kutosha ndani ya uwanja huu, upande wa zimamoto mmenieleza kuwa yapo magari mapya mnayaleta,"
"Nisisitize tuu kwamba mharakishe uagizwaji wa magari haya ili tuendelee kuwa na usalama zaidi kwa maana kwamba inapotokea kuwa kuna tatizo maana pakitokea ajali ya moto itaathiri sio tuu hapa bali ni watu dunia nzima,"amesema Kagaigai
Pamoja na mambo mengine aliutaka uongozi wa uwanja huo kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya Uviko-19 na kuwataka watumishi wa uwanja huo ambao hawajachanja kuchoma chanjo ya Uviko-19 ili kupunguza maambukizi ya ugonjwa huo.
"Sasa hivi tumeona hiki kirusi kimejibadilisha na kinaenea kwa kasi, tuendelee kusimamia yale maelekezo yaliyotolewa na wizara ya afya tuhakikishe wale watendaji ambao hawajachanja wachanje kwasababu ya kupunguza maambukizo na vifo pia vinavyotokana na ugonjwa huu,"amesema Kagaigai
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa uwanja huo, Christina Mwakatobe amesema wameagiza magari mawili ambayo ni ya kiteknolojia ya hali ya juu na yenye vifaa vya Kimataifa kwa ajili ya kuhakikisha usalama katika uwanja huo pale ambapo pakitokea janga la moto.
"Haya magari mawili tunayoenda kupata ni ya kutumia teknolojia ya hali ya juu, kwa hiyo yana vifaa vya Kimataifa na tayari watu wamepata mafunzo kwa ajili ya kutumia magari hayo,"amesema Mwakatobe
Amesema kampuni hiyo ya uwanja wa ndege imenunua mashine 6 mpya za ukaguzi wa mizigo pamoja na abiria.