Ripoti ya CAG yabaini magari 21 yamelipiwa Sh4 bilioni hayajapokelewa

Dar es Salaam. Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka 2021/22 imebaini kuwa taasisi tisa zilinunua magari 21 kupitia kwa Wakala wa Huduma ya Ununuzi Serikalini (GPSA) magari hayo hayajakabidhiwa kwa taasisi ambazo zimenunua.

Ripoti hiyo ya CAG, Charles Kichere iliyowasilishwa jana Alhamisi Aprili 6, 2023 jijini Dodoma ilisema magari yaliyolipiwa Sh4.06 bilioni lakini hayajakabidhiwa kwa wamiliki husika.

“Kanuni ya 242 (i) ya Kanuni za Ununuzi wa Umma za mwaka 2013 iliyorekebishwa mwaka 2016, inaeleza kuwa ambapo upokeaji wa bidhaa unacheleweshwa au unaonekana utacheleweshwa zaidi ya wakati uliowekwa katika mkataba, taasisi nunuzi lazima ipate ripoti na maelezo kutoka kwa wauzaji au mawakala wao. Pia, inaweza kuweka adhabu ya kikomo kama ilivyoelezwa katika mkataba.

“Maoni yangu ni kuwa, kuchelewa kukabidhi magari yaliyonunuliwa, kunakwamisha kufikiwa kwa malengo yaliyotarajiwa, hivyo kuathiri shughuli za usimamizi na ufuatiliaji. Napendekeza menejimenti za taasisi husika zifanye ufuatiliaji wa karibu kwa Wakala wa Huduma ya Ununuzi Serikalini (GPSA) ili kuhakikisha magari yanafikishwa kwa taasisi nunuzi,” imeeleza Ripoti ya CAG.