Sabaya awataja Magufuli, Dk Mpango na Gavana BoT

KUTOKA MAHAKAMANI: Sabaya awataja Magufuli, Dk Mpango na Gavana Bot

Muktasari:

  • Aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya amewataja Hayati John Magufuli, Makamu wa Rais, Dk Philip Mpango na Gavana wa Benki Kuu kuwa walikuwa wanajua operesheni aliyokuwa akiifanya Arusha.

  

Dar es Salaam. Aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya leo Ijumaa Agosti 13, 2021 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha amewataja Hayati John Magufuli, Makamu wa Rais, Dk Philip Mpango na Gavana wa Benki Kuu kuwa walikuwa wanajua operesheni aliyokuwa akiifanya Arusha.

Sabaya amesema hayo wakati akitoa utetezi mbele ya Hakimu mkazi mwandamizi Odira Amworo kuwa alichokuwa anakifanya Arusha Februari 9, 2021 haikuwa operesheni yake ya kwanza kuagizwa na hayati Rais Magufuli 


Akiongozwa na Wakili anayemtetea Mosses Mahuna, wakati alipoanza kujitetea mahakamani hapo amesema kesi hiyo ni ya kutengeneza na yeye hajaiba wala kumtishia mtu yoyote kwa silaha.

Sabaya alisema siku ya tukio Februari 9, 2021 alipomaliza kuongoza kikao cha kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ya Hai, alipokea simu ya Dk Magufuli aliyemwelekeza kazi ya kufanya katika mkoa wa Arusha ambapo pia alipaswa kuwapitia watu wengine wanne katika uwanja wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA), ambapo watu hao walikuwa na maelekezo juu ya kazi hiyo wanayoenda kufanya.

"Hiyo haikuwa kazi ya kwanza kwa sababu miezi michache iliyopita tulipewa zoezi la kukamata mitambo inayotengeneza noti bandia na tulifanikiwa kukamata mitambo na fedha Sh 800 Milioni bandia eneo la Chanika wilaya ya Temeke mkoa wa Dar es Salaam ,Gavana wa BoT anajua na aliyekuwa Waziri wa Fedha kwa wakati huo Dk Philip Mpango, Makamu wa Rais wa sasa pia anafahamu,"