Serikali kuchunguza madai wananchi kuibiwa data, vifurushi na kampuni za simu

Serikali kuchunguza madai wananchi kuibiwa data, vifurushi na kampuni za simu

Muktasari:

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari,  Dk Faustine Ndugulile amelielekeza Baraza la Ushauri la Watumiaji wa Huduma za Mawasiliano (TCRA- CCC) kufanya tathmini ya malalamiko yanayotolewa na wananchi dhidi ya kampuni za simu kuhusu kukatwa na kuibiwa vifurushi ili kupata ufumbuzi wa tatizo hilo.

Dar es Salaam. Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari,  Dk Faustine Ndugulile amelielekeza Baraza la Ushauri la Watumiaji wa Huduma za Mawasiliano (TCRA- CCC) kufanya tathmini ya malalamiko yanayotolewa na wananchi dhidi ya kampuni za simu kuhusu kukatwa na kuibiwa vifurushi ili kupata ufumbuzi wa tatizo hilo.

Dk Ndugulile ametoa maelekezo hayo alipokutana na watendaji wa baraza hilo pamoja na Tume ya Taifa ya Tehama kuangalia utendaji wa taasisi hizo na namna zinavyoweza kusaidia Serikali kwenda na kasi ya maendeleo ya teknolojia.

Kwa mujibu wa waziri huyo,  kumekuwa na  malalamiko mengi ya wananchi kuhusu vifurushi vinavyotolewa na kampuni za simu hivyo ni muhimu kuyafanyia kazi ili ufumbuzi wake upatikane.

 Amesema taarifa alizonazo ni kwamba wananchi wanalalamikia huduma za vifurushi ikiwemo kupunjwa na kutozwa fedha nyingi tofauti na data au muda wa maongezi wanaopewa na kutaka suala hilo kupatiwa ufumbuzi.

Hata hivyo, amewataka wananchi kuitumia vizuri mitandao kwa kuwa sheria zipo na hataki ifike wakati Serikali inaingia kwenye mikinzano na wananchi kwa sababu ya mitandao.

Katibu Mtendaji wa TCRA-CCC,  Mary Msuya amekiri  malalamiko mengi dhidi ya kampuni za simu na kuahidi kutekeleza maelekezo ya waziri ili kutatua changamoto wanazokumbana nazo.