Serikali kutenga bajeti ya Kilimo hai 2022

Muktasari:

  • Serikali ya Tanzania na Mapinduzi Zanzibar, zimeazimia kutenga bajeti kwa ajili ya kuendeleza kilimo hai nchini.

Dodoma. Serikali ya Tanzania na Mapinduzi Zanzibar, zimeazimia kutenga bajeti kwa ajili ya kuendeleza kilimo hai nchini.

Serikali hizo zimeazimia pia kutenga bajeti hiyo katika Mwaka wa Fedha ujao.

Naibu Waziri wa Kilimo wa Tanzania, Hussein Bashe amesema Wizara kwa kushirikiana na Wadau wa kilimo nchini, wataanzisha pia benki ya Mbegu kwa lengo la kuendelea kuhifadhi mbegu mbalimbali za asili zitakazomsaidia mkulima kutekeleza kilimo hai chenye uhakika

Bashe ameyasema hayo leo Alhamisi Oktoba 21, 2021 Jijini Dodoma alipokuwa akifungua Kongamano la Kilimo Hai linalowakutanisha wadau wa kilimo na wakulima sambamba na wafugaji kutoka maeneo mbalimbali nchini.

"Kilimo hai ni jambo ambalo halikwepeki, wizara tutaunda kitengo kitakachoshughulikia masuala ya kilimo hai na mwaka ujao wa fedha tutatenga bajeti "amesema Bashe.

Ameongeza "Sisi kama wizara katika nchi hii ni lazima tuanze mchakato  wa kuanzisha benki kubwa ambayo itakuwa kwa ajili ya kusafisha mbegu,kuzalisha mbegu za asili  ili ziweze kupatikana kwa wingi kwa ajili ya wakulima wetu ,"amesema Bashe.