Serikali kuvilipa vyombo vya habari Sh6 bilioni

Serikali kuvilipa vyombo vya habari Sh6 bilioni

Muktasari:

  • Rais Samia Suluhu Hassan amesema serikali itavilipa vyombo vya habari deni la zaidi ya Sh6 bilioni baada ya kufanya uhakiki wa deni hilo ambalo ni moja ya mambo yaliyosababisha kufa kwa baadhi ya vyombo hivyo.


Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan amesema serikali itavilipa vyombo vya habari deni la zaidi ya Sh6 bilioni baada ya kufanya uhakiki wa deni hilo ambalo ni moja ya mambo yaliyosababisha kufa kwa baadhi ya vyombo hivyo.

Rais Samia ametoa ahadi hiyo leo Jumatatu Juni 28, 2021  jijini Dar es Salaam wakati akijibu swali la mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile aliyemuomba kiongozi mkuu huyo wa nchi kutimiza ahadi iliyotolewa na Waziri Mkuu, Kassimu Majaliwa ya kulipa deni hilo kabla ya Juni 30, 2021.

Amesema Serikali itafanya uhakiki wa madeni hayo ya vyombo vya habari, kIsha itaanza kulipa kidogokidogo mpaka deni hilo liishe.

“Nitafanya kazi na waziri mkuu katika kuhakikisha kwamba tunalipa madeni haya kidogokidogo lakini lazima tuyafanyie uhakiki kisha tuweze kulipa, hatutaweza kulipa kwa mkupuo,” amesema.

Kuhusu katazo la Serikali kutangaza kwenye vyombo vya habari, Rais Samia amesema tangu ameingia ofisini, hajaona kama kulikuwa kuna katazo hilo hata hivyo katika utawala wake hakutakuwa  na katazo hilo.

“Wakati wangu huu sitakataza matangazo kwenye vyombo binafsi, kwa hiyo ni jukumu letu kutafuta matangazo hayo,” amesema Rais Samia.