Serikali kuweka kumbukumbu ya Rais Museven, Magufuli ujenzi shule Chato


Muktasari:

Rais Samia Sulhu Hassan ameiagiza Elimu, Sayansi na Teknolojia kuweka kumbukumbu ya ujenzi wa shule ya Msingi Museven katika maktaba ya shule hiyo ikiwa ni historia ya Rais wa Uganda, Yoweri Museven na aliyekuwa Rais wa Tanzania, Hayati Dk John Magufuli.

Chato. Rais Samia Sulhu Hassan ameiagiza Elimu, Sayansi na Teknolojia kuweka kumbukumbu ya ujenzi wa shule ya Msingi Museven katika maktaba ya shule hiyo ikiwa ni historia ya Rais wa Uganda, Yoweri Museven na aliyekuwa Rais wa Tanzania, Hayati Dk John Magufuli.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano ya shule hiyo iliyofanyika wilayani Chato Mkoa wa Geita leo Novemba 29, 2021, Rais Samia amesema ameagiza hivyo ili watoto watakaosoma shuleni hapo wajue chanzo cha shule hiyo na kuelewa historia ya viongozi hao waliodhamilia na kutimiza ujenzi wa shule hiyo.

“Lakini pia wanafunzi wetu watakaojifunza hapa waelewe falsafa za viongozi wetu za uzalendo za Rais Magufuli na falsafa za Rais Museven kuhakikisha waafrika wanajitegemea kwenye sekta za kiuchumi, kijamii na kisiasa,”amesema

Amemuomba Rais Museven kama ikimpendeza shule hiyo ipate shule pacha nchini Uganda ili wanafunzi waweze kubadilishana uzoefu na kutembeleana.


Rais Samia amesema Serikali itahakikisha shule hiyo inakuwa na kiwango kama alichotarajia Hayati Magufuli kwa kuongeza mabweni ya wanafunzi, kuongeza nyumba za walimu watakaokuwa wanafundisha na kutengeneza vizuri barabara na mazingira ya shule hiyo.

“Nikuahidi Rais na niwaahidi wana Chato wenzangu, kwamba kazi hiyo sasa tunaibeba Serikali kuweka mazingira na kumalizia pale palipobaki ili shule hii ifikie viwango vile ambavyo marehemu alitarajia kufikisha,”amesema na kuongeza

“Serikali ya Tanzania itaendelea na ujenzi wa miundombinu ya shule za msingi za serikali nchini kwa kushirikiana na wananchi pamoja na wadau mbalimbali wa elimu wa ndani na nje ya nchi; makabidhiano yanayofanyika leo yanatia chachu kwa serikali kuhakikisha inatoa elimu bora na kwa usawa kwa watoto wote wa Tanzania,”