Serikali ya Tanzania yaeleza mkakati kuchochea uchumi shindani

Serikali ya Tanzania yaeleza mkakati kuchochea uchumi shindani

Muktasari:

  • Serikali imesema katika kuchoche uchumi shindani na shirikishi, msukumo utawekwa katika miradi inayolenga kuwa na utulivu wa uchumi.

Dar es Salaam. Serikali imesema katika kuchoche uchumi shindani na shirikishi, msukumo utawekwa katika miradi inayolenga kuwa na utulivu wa uchumi.

Hayo yamesemwa leo Alhamisi Juni 10, 2021 na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba wakati akiwasilisha bungeni hali ya uchumi wa Taifa kwa mwaka wa fedha 2020/21 na mpango wa maendeleo ya Taifa kwa mwaka wa fedha 2021/2022.

“Katika kuchoche uchumi shindani na shirikishi, msukumo utawekwa katika miradi inayolenga kuwa na utulivu wa uchumi na uendelezaji wa reli, barabara, madaraja, usafiri wa majini, anga, nishati, bandari, viwanja vya ndege pamoja na utekelezaji wa mpango kazi wa kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji,” amesema Dk Mwigulu.

Amesema katika eneo hilo miradi ifuatayo itapewa uzito ikiwemo uendelezaji wa miundombinu ambapo amesema mradi wa reli katika mwaka wa fedha 2021/22 kutakuwa na ukarabati wa njia ya kuu za reli, matengenezo ya njia za reli, karakana na majengo ya reli, vichwa vya treni na ukarabati wa mabehewa.

Dk Mwigulu amesema msukumo pia utawekwa katika barabara za lami zinazofungua fursa za kiuchumi nchini, barabara za mikoa, barabara ziendazo kasi, barabara za mzunguko jiji la Dodoma, barabara za juu na zile za mijini na vijijini yaani Tarura.

“Katika usafiri wa majini Serikali itajenga na kukarabati gati katika maziwa makuu kuboresha bandari zote hasa Bandari ya Dar es Salaam. Kwa upande wa usafiri wa anga ni maboresho ya jengo la pili la abiria, kuboresha viwanja vya ndege, Songwe, Msalato na viwanja vingine vya mikoa ya Kigoma, Sumbawanga na Shinyanga,” amesema Dk Mwigulu.