Serikali yaja na mbinu mpya usimamizi mikopo asilimia 10
Dododma. Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Innocent Bashungwa amesema Serikali itaimarisha usimamzi wa utaoji wa mikopo ya asilimia 10 kwenye halmashauri kwa kutumia mifumo ya Tehama ili mikopo hiyo iweze kuwanufaisha wahusika na kuleta mabadiliko chanya kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.
Waziri Bashungwa ameeleza hayo leo Ijumaa Juni 24, 2022 bungeni jijini Dodoma wakati akichangia mjadala wa bajeti kuu ya Serikali ya mwaka wa fedha 2022/23 na kueleza kuwa mfumo wa kielektroniki utasaidia kuongeza usimamizi kwa kutambua anayepewa mkopo, shughulli anayoifanya na urejeshaji wa mkopo katika halmashauri zote nchini.
“Tutasimamia Sheria za utoaji wa mikopo ya asilimia 10 na kuhakikiha kila Mkurugenzi anatoa mikopo hiyo kwa wakati na sio kwa hiari bali ni takwa la sheria na kuzingatia utawala bora katika usimamizi wa mikopo hiyo” amesema Bahungwa.
Bashungwa amesema moja ya kigezo kitakachotumika kupima ufanisi wa wakurugenzi katika halmashauri ni usimamizi wa utoaji na urejeshaji wa mikopo ya vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.
Amesema Serikali itaimarisha nidhamu katika Tawala za Mikoa na Serikali za mitaa na kuhakikisha wakuu wa mikoa, wilaya na wakurungenzi wa Halmashauri wanatoa ushirikiano kwa wabunge ambao ni watetezi na wawakilishi wa wanannchi.
Amesema Tamisemi inaendelea kuzifanyia kazi changamoto mbalimbali zilizopo kwenye baadhi ya halmashauri na kuzipati ufumbuzi wa haraka lengo likiwa ni kuhakikisha huduma bora inatolewa kwa wananchi